Ni miaka 76 tangu kulipuka kwa bomu la Atomiki huko Nagasaki!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Mji wa Nagasaki nchini Japan tarehe 9 Agosti limefanya kumbukumbu ya miaka 76 tangu uliposhambuliwa kwa bomu la nyuklia na Marekani siku tatu baada ya lile la Hiroshima lililolipuka yarehe 6 Agosti 1945. Maaskofu wa Marekani kwa mara nyingine tena wanasisitiza wito wao kuhusu shinikizo dhidi ya kuongezeka kwa nyuklia, kwa maneno mazito yaliyosemwa na Papa Francisko alipotembela huko Nagasaki na Hiroshima wakati wa ziara yake ya kitume nchini Japan kunako tarehe 24 Novemba 2019.
Papa alikwenda Japan kama mhujaji wa amani, hija ambayo ameihifadhi katika moyo wake na alikazia kusema kwamba, katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, anabeba kilio cha maskini ambao daima wamekuwa ni waathirika wakuu wa kinzani, mipasuko mbali mbali pamoja na vita. Hata hivyo Papa Francisko wakati wa ziara yake alisisitiza kuwa ili kuweza kuwa na amani ya kudumu, kuna haja kwa watu wote kuweka silaha zao chini, lakini zaidi zile silaha ya maangamizi yaani: silaha za nyuklia zinazoweza kuleta maafa makubwa zaidi kwa miji na nchi mbali mbali duniani.
Papa aidha alionya kuwa ulimbikizaji na matumizi ya silaha za atomiki kwa ajili ya vita ni kinyume cha maadili na utu wema. Na kwa maana hiyo Papa amekuwa na matumaini kuwa ushuhuda wa “hibakusha” yaani wahanga wa mashambulizi ya mabomu ya nyuklia huko Hiroshima na Nagasaki utaendelea kuwa ni sauti inayotoa onyo kwa Jumuiya ya Kimataifa na kwa kizazi kijacho.