Hawa ni baadhi ya waandamanaji wa Mali wakipeperusha bendera za Mali na Urusi Hawa ni baadhi ya waandamanaji wa Mali wakipeperusha bendera za Mali na Urusi 

Mali:Maaskofu watoa wito wa mazungumzo ya kujenga na si kubomoa

Baraza la Maaskofu nchini Mali(Cem)wanalaani vikali mapinduzi ya kijeshi yaliyotkea hivi karibuni nchini humo na kwa maana hiyo wanatoa wito wa kufanya mazungumzo ya kujenga na siyo ya kubomoa.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Katika tukio la mapanduzi ya kijeshi huko Mali, yaliyotokea hivi karibuni, Baraza la Maaskofu katoliki (Cem) nchini humo wamelilaani na kutoa maoni yao kwa wito wa kufanya mazungumzo ya kujenga na siyo kubomoa.  Hili ni tukio la Jumatatu jioni, wiki hii ambapo mapinduzi mapya ya kieshi yalifanyika katika taifa la Kiafrika, miezi tisa tu baada ya lile la awali, kwa maagizo ya Kanali, Assimi Goita aliyekuwa makamu wa rais baada ya kuongoza mapinduzi mwezi Agosti mwaka uliopita na kumuondoa madarakani Rais Ibrahim Boubacar Keita. Ndaw na Waziri Mkuu, Moctar Ouane ambao walishikiliwa baada ya mapinduzi hayo walijiuzulu siku ya Jumatano, wakiwa bado kizuizini. Viongozi hao waliokuwa katika serikali ya mpito waliachiwa huru siku ya Alhamisi. Hayo ni mapinduzi ya pili kufanyika Mali ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.

Maaskofu kwa maana hiyo wanaonesha kukasirika kwa kile kinachotokea kwa sasa na wamerudia kuelezea uhitaji wa mtendaji mwenye nguvu na jeshi lililopatanishwa na kuimarishwa, huku wakilaani kabisa mgogoro wa sasa uliotokana na masuala ya ubinafsi, mbali na wasiwasi wa watu na masilahi ya nchi ya Mali. Idadi ya watu, kwa dhati wanakabiliwa na changamoto mbali mbali za shida kubwa, pamoja na usalama, afya na masuala ya kijamii na kiuchumi, wakati wafanyakazi wako kwenye mgomo wakiomba haki zao zitambuliwe.

Katika haya yote, Maaskofu wa mali (Cem) wamebainisha kuwa nchi inakabiliwa na mabadiliko ya kisiasa ambayo yamejadiliwa kwa shida sana na jumuiya ya kimataifa ambayo kwa ujumla inajaribu kurudisha taifa kwenye njia ya demokrasia. Kwa maana hiyo wito wa maaskofu ni kufanya mazungumzo ya kujenga ili kumaliza mgogoro wa sasa na kujaribu kufikia mapatano ya kijamii ili kuweza kujenga, kwa msaada wa Mungu, amani na udugu. Kwa kuhitimisha Maaskofu wa Mali wanaandika kuwa: “Bwana awapatie viongozi wetu na raia wote hekima na dhamiri zinazo hitajika ili kutafuta hasa wema wa wote na ili nchi iweze kuendelee na safari yake katika ukweli, maelewano, ustawi, haki na amani".

Hata hivyo Mahakama ya Katiba ya Mali Jumamosi tarehe 29 Mei imemtangaza Kanali Assimi Goita kuwa rais mpya wa mpito kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Rais Bah Ndaw ambaye amejiuzulu. Katika uamuzi wake mahakama hiyo imesema Goita aliyeongoza mapinduzi ya kijeshi siku ya Jumatatu anapaswa kujaza nafasi hiyo. Uamuzi huo unazidisha kukwama ambapo viongozi wa mataifa ya Afrika Magharibi walikuwa wanajiandaa kukutana siku ya Jumapili tarehe 30 Mei 2021 kuzungumzia juu ya hatua ya kukabidhi madaraka, ambayo inahatarisha harakati za kuelekea kwenye demokrasia na kudhoofisha mapambano dhidi ya wapiganaji wa kijihadi katika ukanda huo uliogubikwa na ghasia.

29 May 2021, 15:33