Iraq:Moto waunguza Hospitali ya Baghdad.Ni janga la kibinadamu
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Akizungumza kuhusiana na janga la mlipuko wa moto katika hospitali ya Ibn al-Khatib yenye wagonjwa wa Covid huko Kusini Mashariki wa Mji wa Baghdad, nchini Iraq, Kardinali Louis Raphael Sako, Patriaki wa Babilonia ya Wakaldayo nchini Iraq, ameandika kuwa "Hili ni balaa la kibinadamu na kitaifa ambalo linahitaji wote kuungana kwa pamoja na kuonesha mshikamano". Moto ulisambaratika sana katika usiku kati ya tarehe 24 na 25 Aprili 2021 na kusababisha karibu vifo vya watu 82 na zaidi ya majeruhi 100. Kati ya wagonjwa waliokufa wengi wao walikuwa kwenye viumba mahututi. Ni tukio ambalo limeibua uchungu mkubwa sana na huzuni kwa mjibu wa Kardinali, huku akiwa na matumaini kwamba ushirikiano kwa wote utakuwapo kwa pamoja ili kuchukua hatua za lazima ya kuzuia majanga ya namna hiyo ya aibu yasitokee tena.
Papa awaombea waathiriwa 82 wa moto katika hospitali ya Baghdad
Papa Francisko Jumapili tarehe 25 Aprili 2021 mara baada ya sala ya Malkia wa Mbingu ameomba sala kwa ajili ya waathiriwa nchini Iraq katika usiku wa kuamkia Jumapili kutokana na Hospitali ya wagonjwa wa Covid, huko Baghadad kuungua moto. Alisema kuwa hadi sasa ni watu 82 waliokufa na majeruhi katika tukio hilo.
Jitihada za Kanisa pamoja na serikali
Kardinali Sako akielezea mkasa huo amesema kama Kanisa wanahakikisha jitihada zao kamili pamoja na nguvu za serikali, vyombo vya madola na watu wa huduma ya kiafya na wote wenye wenye mapenzi mema katika kujenga amani na msimamo na kutoa huduma msingi kwa watu, hasa katika hali halisi ngumu ya sasa ambayo imeletwa na janga na mizozo. Hatimaye Kardinali Sako, ameinua sala zake kwa Mungu ili kuwaombea marehemu wote wapumzike kwa amani na kwa ajili ya uponywaji wa majeruhi hao na Iraq iweze kuinuka kutokana na migogoro ya sasa.
Kardinali alitembelea hospitali ya Ibn Al-Khatib
Kwa mujibu wa taarifa ni kwamba Kardinali mwenyewe, Jumapili tarehe 25 Aprili alikwenda kutembelea Hospitali hiyo ya Ibn Al-Khatib, mahali ambapo alipokelewa na wakuu wa hospitali hiyo ambao walielezea juu ya janga hilo. Kwa maana hiyo Kardinali Sako aliwasha baadhi ya mishumaa na kusali sala kwa ajili ya marehemu, majeruhi na familia zao. Kwa mujibu wa Kardinali amesitizia jitihada za Kanisa ili kupata msaada wa kifedha kwa ajili ya watu waliokumbwa na mkasa wa moto kwa ushirikiano na mamlaka.