Myanmar.Kard.Bo ahimiza wakristo wawe manabii wa amani
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Rais wa Baraza la Maaskofu nchini Myanmar (CBCN) Kardinali Charles Maung Bo katika ujumbe wake uliotolewa tarehe 18 Januri 2021 katika fursa ya Wiki ya kuombea Umoja wa Kikristo (18-25 Januari, amesema kuwa kuna dharura ya mahitaji ya chanjo ya amani, Wakristo wote wanapaswa kuungana na kusikiliza maneno ya Bwana wetu “ninawachia amani, ninawapa amani”.
Majanga ya sasa nchini Myanmar
Kardinali Bo katika ujumbe huo amesema vita vya miongo saba ni janga. Maelfu ya watu wanaoishi katika kambi duni ni janga. Dawa za kulevya na uporaji wa rasilimali zao ni janga. Vizazi vimepata vita visivyo na mwisho, ameongeza kusema kuwa vita hivi havikutoa suluhisho lolote la matatizo kwa miongo kumi. Kwa maana hiyo anawalika Wakristo kuwa manabii wa amani nchini Myanmar iliyokumbwa na mizozo, iliyosumbuliwa na miongo kadhaa ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, ambapo amani bado haipo wakati mapigano ya hapa na pale yanaendelea kupamba moto katika majimbo ya Karen, Shan na Rakhine.
Wito wa kuungana ili kukabiliana na changamoto
Kwa mujibu wa Kardinali Bo anasema ni kwa kuungana pamoja tu, wanaweza kweli kukabiliana na kushinda changamoto za maisha kama walivyofundishwa hata na janga hili la kiafya ambalo limesababishwa na kuendelea kusambaa kwa virusi vya corona. Umoja ndiyo nguvu yao na wito wao; Amani inawezekana na amani ndiyo njia moja pekee. Waungane kwa pamoja kuzungukia altare ya nchi yao takatifu na kugawana mkate wa amani. Kwa kuungana amesisitiza Kardinali Bo kuwa ndipo Mungu atawapatia hekima kwa ajili ya kushinda tofauti zao na kuwabariki katika kutafuta amani bila kuteteleka.