Morocco:waamini watiwa moyo kuanza upya mwaka wa kichungaji!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Katika barua ya Kardinali Cristóbal López Romero, Askofu Mkuu wa Rabat, nchini Mrorocco katika fursa ya kila mwaka kuwaandikia waamini wake barua ya kichungaji anagusia kwa karibu sana juu ya ukosefu wa usalama kwa upande wa kiafya a kutokana na hali halisi ya virusi vya corona au covid-19 na zaidi baada ya kufungua kwa mara nyingine tena shughuli taratibu katika nchi yao. Barua yake inasema: “Tunapaswa kuwa na uvumilivu na wabunifu, kama jinsi ambavyo tumekuwa hivyo. Lazima kujua namna ya kuendana na hali halisi itakavyokuwa na kufanya kile ambacho tunatakiwa kufanya au ulazima wa kufanya. “Ikiwa leo hii haiwezekani basi itakuwa kesho; ikiwa tunaweza kufanya kwa namna hiyo, basi tutafanya kwa njia tofauti, lakini maisha ya jumuiya zetu lazima yaendelee.”
Kardinali katika barua hiyo aidha anasema “tumefanya uzoefu wa aina nyingine za mwasiliano na maadhimisho, tumeishi kidugu kwa njia tofauti na tumeongezea shughuli za mshikamano na ushirikishano”, na kusisitiza juu ya miezi ya karantini wakati huo huo akiwatia moyo juu ya kujenga mawazo mapya kwa namna ya pekee katika Kipindi cha kazi ya Uumbaji (Season of Creation), tukio la kila mwaka ambalo linahamasisha maombi ya sala na utunzaji wa Mazingira nyumba yetu ya pamoja. Ni kipindi kinachoanzia tarehe 1 Septemba hadi kufikia tarehe 4 Oktoba sambamba na Siku kuu ya Mtakatifu Francis wa Assisi msimamizi wa Mazingira. Hatimaye Askofu Mkuu wa Rabat, anawashauri waamini kuandaa shughuli za kichungaji, maandalizi ya ukatekumeni na katekesi, kuanza mwezi Oktoba mwaka huu kwa kuwa na mwanga mpya wa mwanzo wa mwaka mpya wa kichungaji jimbo kuu lao.