2020.06.30 Padre  Edwin Mulandu Mkurugenzi wa PMS  nchini Zambia. 2020.06.30 Padre Edwin Mulandu Mkurugenzi wa PMS nchini Zambia. 

Zambia-Mkurugenzi PMS:Njia mpya zinahitajika katika utume wa kimisionari!

Ni muhimu kuanza mipango mingine ya uhamasishaji na malezi ya wamisionari kwa faida ya waamini wote ili waweze kujifunza zaidi juu ya shughuli za Kipapa za utume wa kimisionari.Ni kwa mujibu wa Padre Edwin Mulandu,Mkurugenzi wa Kitaifa wa kazi za kimisionari wa Mashirika ya kipapa (PMS) nchini Zambia,katika mahojiano hivi karibuni kuhusu Ujumbe wa Papa alioutuma kwa Shirika la Kipapa la Kazi za kimisionari tarehe 21 Mei 2020.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Ingawa dharura ya Covid-19 mwaka huu imetuzuia kukutana na Baba Mtakatifu moja kwa moja katika Mkutano Mkuu ufanyikao kila mwaka ambao umewekwa  kwa ajili ya Mashirika ya Kipapa ya Kazi za kimisionari, hisia  zangu zilikuwa sawa na zilinigusa sana kwa kupokea ujumbe wake. Tulisikia uwepo wake na ukaribu sana. Hayo yamesemwa na Padre Edwin Mulandu, Mkurugenzi wa Kitaifa wa kazi za kimisionari wa Mashirika ya kipapa (PMS) nchini Zambia, katika mahojiano na shirika la habari za kimisionari  Fides, hivi karibuni akitoa maoni kuhusu Ujumbe ambao Papa Francisko alioutuma kwa Shirika la Kipapa la Kazi za kimisionari (PMS) kunako  tarehe 21 Mei 2020, katika  siku  kuu ya Kupaa kwa Bwana.  

Akijibu swali kuhusiana na jambo lipi ambalo lilimegusa katika ujumbe huo anasema “Ujumbe wa Papa  umefanyiwa kazi nzuri sana na unasisitiza mambo mengi na zaidi:  msingi wa upendo wetu kama  chombo cha huduma ya kipapa ya  kimisionari  ambayo ni Huduma kwa Kanisa na kwa Papa mwenyewe; utambulisho wetu wa umisionari; sala  na upendo kama njia rahisi ya kushiriki katika utume wa kimisionari. Aidha amesema kwamba aliguswa wakati Papa aliongea juu ya kuhifadhi na kurudisha jukumu la shirika la Kipapa la Kazi za Kimisionari (PMS) kwani hata katika miaka iliyopita, Papa alirudia kuwakumbusha hatari ya kubadilisha Shirika la PMS kuwa shirika lisilo la kiserikali (NGOs). Hii ina maana hasa katika ambazo juhudi zao zote zinajitoa katika ukusanyaji  na kusambaza fedha kama hakuna uangalifu. Kwa kufafanua suala hili amesema “Wakati mwingine tunahatarisha kutumia njia za kitaalam za kutafuta fedha lakini ambazo hutumiwa na mashirika yasiyo ya kiserikali( NGOs) na ambazo haziendani na karama ya PMS. Kila kazi tunayofanya lazima iwekwe mikononi mwa Bwana. Pia ninaona ni muhimu sana ukweli kwamba Papa katika ujumbe wake anasisitiza kuhusu hitaji la kuwa makini kwa mahitaji msingi ya jamuiya, huku tukiepuka utamaduni wa ustawi, ambao badala ya kusaidia bidii ya umisionari, huishia kufanya mioyo kuwa mizito na ya uvuguvugu na kuongeza  matukio ya ulevi,

Kwa upande wa ufafanuzi wa ujumbe wa  Papa utakavyosaidia kupyaisha PMS nchini Zambia amesema “ni muhimu kuanza mipango mingine ya uhamasishaji  na malezi ya wamisionari kwa faida ya waamini wote ili waweze kujifunza zaidi juu ya shughuli za  Kipapa za utume wa kimisionari. Katika muktadha wao, kwa mfano, PMS kwa walio wengi inajulikana kama shirika la ufadhili wa kifedha kwa sababu shughuli yao inahusika  sana na miradi. Na kwa walio wengi Mkurugenzi wa PMS anatambuliwa zaidi kama meneja wa mradi, kama kuhani anayesimamia miradi. Kwa upande wake anabainisha kwamba “Changamoto ni ile ya kuingia kwa dhati katika maisha ya watu ya kila siku, kuwashirikisha makuhani wa parokia, watawa wa kike na kiume waliowekwa katika shughuli za utume wa Shirika la Kipapa la  kazi za  kimisionari (PMS)”. Njia nyingine muhimu ya utume nchini Zambia ni kwamba inawakilishwa na umaskini. Inahitaji kuzingatia juhudi ili parokia kubwa katika miji mikubwa iweze kutoa msaada mkubwa kwa parokia zilizo duni katika vijiji vyao na kutia moyo roho ya ushiriki kati ya waamini. Wakati mwingine, kuna tabia ya kupokea bila kufanya chochote, amelalamika. Tabia hii lazima izuiwe kabisa! Lazima kuunda akili ambayo kwa kiasi kikubwa ina maono kwa ngazi ya kubadilishana na kutoleana zawadi. Hata sala kwa ajili ya wale ambao wanahusika moja kwa moja katika shughuli za kimisionari na ambao wanatakiwa watiwe moyo na waamini wote kama mtindo mwema wa kushirikishana na unaowarudisha pamoja katika shughuli  zote za kimisionari.

Hatimaye mkurugenzi huyo amejibu swali kuhusu mtazamo wa PMS katika Kanisa nchini mwake na ulimwenguni  kwamba akitafakari wakati ujao wa PMS anafikiria umuhimu wa kutazama wakati uliopita na uliopo. Kwa maana ya kwamba lazima kufanya zaidi yaani kujikita zaidi katika rasilimali watu na wakati wa mafunzo. Karama  za waanzilishi wa kazi za  kimisionari zinapaswa zichukue jukumu kubwa katika malezi yetu ya umisionari. Sala na upendo kila wakati vinapaswa kwenda pamoja kwenye Uhamasishaji wa shughuli za kimisionari. Vikundi vya uhamasishaji wa kimisionari na zile zinazohimiza ukusanyaji wa fedha zinapaswa kuzingatia kwa karibu kuhusu sala na malezi. Pia, amefikiria shughuli za Utoto Mtakatifu  ambao ni chanzo cha tumaini kubwa kwa siku zijazo  nchini Zambia na katika  ulimwengu wote. Malezi yao ya kimisionari yamekamilika amesisitiza. Watoto huelimishwa katika sala na sadaka ya vitu kulingana na kauli mbiu yao isemayo “Watoto ambao husaidia watoto”, inafupisha karama ya matendo yao yote. Kwa maana hiyo wanalo tumaini kubwa kwamba watoto hawa, baada ya malezi yao, watakuwa wahudumu wa kujitoa sana na siyo tu katika Utoto Mtakatifu,  bali ndani ya Jumuiya nzima ya Wamisionari wa kipapa. Kama vile Papa Francisko alivyoandika katika ujumbe wake akimnukuu Mtakatifu Ignatius wa Loyola, “tunachostahili kufanya ni kufikiria kufanya kazi yetu vizuri, kana kwamba kila kitu kinategemea sisi, ingawa tunajua kuwa kila kitu kinategemea Mungu.”

Ikumbukwe Mashirika ya Kipapa ya kimisionari ni vyombo muhimu katika uhamasishaji wa kazi za kimisionari ambayo ni kwa ushirikiano mkubwa sana wakiongozwa na Mkuu wa Kanisa la Roma ambaye ni Papa. Jukumu kuu la Mashirika haya ni kuhamasisha roho ya kimisionari miongoni mwa familia ya Mungu katika  kuelekeza, kuratibu na kuhamasisha shughuli za uinjilishaji wa kina kwa waaamini wote kama vile kutoa mafunzo ya kimisionari; kukuzaji na kuimarishaji wa malezi na miito mbali mbali ndani ya Kanisa. Kila kona ulimwengu wapo Wakurugenzi wa Mashirika ya Kipapa kitaifa ambao utaribu shughuli zote za kimisionari ndani ya Taifa lao, hatimaye kuweza kutoa mrejesho wa kweli kwa makao makuu ya kwa Shirika la Kipapa la Kimisionari (PMS). Wakurugenzi wa Mashirika ya Kipapa wanafanya huduma yao kwa kutumia njia mbali mbali hasa za wkati huu kama vile za kisayansi na teknolojia ya mawasiliano kuwafikia waamni wengi iwezekanavyo hasa katika kuhamasisha uchangiaji wa shughuli hai za utume wa Kanisa. Pamoja na hayo wakurugenzi ushirikiana sana na wahusika wa maparokia, vyama vya kitume na watawa ili kurahisha shughuli zao za kitume.

30 June 2020, 11:45