Ecuador:wasiwasi wa Kanisa kuhusu uhalishwaji wa utoaji mimba
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Maaskofu nchini Ecuador wanatoa wito kwa waamini ili kuomba, kutafakari na kushiriki kikamilifu katika matendo ya dhati ya utetezi wa maisha hai ya mwanadamu, kufuatia na matazamio ya mjadala wa bunge juu ya uamuzi wa mada za utoaji wa mimba katika kesi ya ukiukwaji, kiumbe kukaa vibaya tumboni, ubakaji, uzinifu na upandaji wa mbegu za uzazi usio idhinishwa. Maaskofu katoliki wanasema hizi ni mada nyeti sana na ngumu na ambazo zinahitaji ushiriki wa kidhamiri na ari ya kila mmoja katika sababu hizo.
Hii ni taarifa kutoka kwa maaskofu katoliki ambao wanasisitiza kupitia Gazeti Katoliki la Sir juu ya suala hili muhimu la maisha ya binadamu hasa katika utetezi wa maisha. Aidha wanasema kuwa tatizo la kutokujali na ugumu wa kusikia, kwa wakristo ni dhambi kubwa sana. Kwa sababu hiyo, maaskofu wanapenda kuwaalika wanaume na wanawake wote wanaopenda maisha ili kuungana kwa pamoja katika siku ya sala, tafakari na katika kufanya matendo ya dhati ya utetezi wa maisha hai ya mwanadamu.
Uhamasishaji wa siku ya maombi
Maaskofu katoliki nchini Ecuador kwa namna ya pekee wanashauri waamini wao kuwa katika siku ya maombi, maparokia yote, jumuiya za kidini, taasisi katoliki za walei, kuhamasisha siku ya sala kwa ajili ya kukuza maisha yanayozaliwa na wazazi wao. Kadhalika Maaskofu wanawataka waamini wawe na hali ya heshima na kuendeleza kuandaa mijadala na mikutano hasa na vijana, kwa kuhamasisha tafakari na malengo yake juu ya suala hilo nyeti katika taifa lao. Na katika ngazi ya kimatendo, maaskofu wanasisitiza kuwa jitihada ziwe ni zile za kuendeleza kutangaza kama wazalendo na waamini wanaokuza maisha kwa namna iliyo wazi na moja kwa moja, katika kujikita kwenye mazungumzo na viongozi wa kijamii na kisiasa katika hali ya amani!
Jitihada ya kukuza maisha
Hata hivyo ni lazima kukumbuka kwamba miezi ya hivi karibuni, maaskofu wa Ecuador walikuwa wameelezea juu ya umuhimu wa kulinda maisha, kutungwa kwake hadi kifo cha kawaida. Katika taarifa zilizo sambazwa mwezi Januari mwaka huu, kwa mfano, maaskofu walikuwa wameandika: "Maisha ya mwanadamu ni yenye thamani ya juu kuliko kitu chochote na zaidi ya mipango yoyote iwe kisiasa au kidini, au nafasi zilizo hitimu kama vile za wadau au wanamaendeleo. Kwa sababu hiyo, walikuwa wanawakumbusha juu ya mahitaji ya kuhakikisha kiwango cha maadili katika maisha ya mwanadamu, hasa kutunza hadhi na uhuru wa mwanadamu.