Prof. Costa Ricky Mahalu, Makamu Mkuu Chuo Kikuu cha SAUT
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Askofu mkuu mteule Gervas J. M. Nyaisonga, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, TEC, kwa madaraka aliyo nayo kisheria kwa mujibu wa Katiba ya Chuo ya Mwaka 2010, amemteua Profesa Costa Ricky Mahalu kuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania. Uteuzi huu unaanza tarehe Mosi, Machi 2019. Profesa Mahalu, Balozi na Mwanasheria aliyebobea anachukua nafasi ya Padre Thadeo Mkamwa, ambaye amekwenda masomoni ili kuongeza ujuzi na maarifa zaidi. Nafasi hii kwa muda imekuwa ikishikiliwa na Profesa Gabriel Mbaga.
Askofu mkuu mteule Nyaisonga amefafanua kwamba, kabla ya uteuzi huu, Profesa Costa Rick Mahalu alikuwa ni miongoni mwa wakufunzi wa Chuo Kikuu cha SAUT kinachoendeshwa na kumilikiwa na Kanisa Katoliki nchini Tanzania! SAUT ni Chuo Mama kati ya Vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania! Ni matumaini ya Dr. Negussie Andre Dominic, Makamu Mkuu wa Chuo, Utawala na Fedha kwamba, Jumuiya ya Chuo Kikuu cha SAUT itampatai ushirikiano wa kutosha Profesa Mahalu ili aweze kutekeleza vyema shughuli zake!