Bi Samia Suluhu ni mwanamke wa kwanza kuwa rais Tanzania
Na Sr. Angela Rwezala- Vatican.
Pamoja na majonzi makubwa, na mshangao nchini Tanzania kufuatia na kifo cha aliyekuwa mpendwa wa nchi rais John Pombe Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi, jijini Dar Es Salaam, leo hii tarehe 19 Machi 2021, Bi Samia Suluhu Hassan mwenye umri wa miaka 61 na aliyekuwa ni makamu wake, ameapishwa katika ikulu ya jijini Dar es Salaam kuchukua wadhifa huo. Anawakuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais nchini Tanzania , lakini pia kwa kanda ya Afrika Mashariki na wa pili kwa Afrika maana wa kwanza ni nchini Ethiopia.
Mara baada ya kula kiapo na kukagua gwaride lililoambatana na mizinga ikiwa ni utaratibu wa kawaida kama amri jeshi mkuu, Bi Samia amehutubia taifa kwa kuanza kutoa taratibu za mazishi ya hayati Rais Magufuli, ambapo maombolezo yatakuwa ni siku 21 na kuelekeza kuwa, marehemu ataagwa kuanzia Dar es Salaam na kufuatiwa na mkoa Dodoma na Mwanza kuwakilisha mikoa yote kabla ya kuzikwa nyumbani kwao kufuatia Chato kuafuatia na uamuzi wake. Aidha Bi Suluhu amelitangazia taifa lake siku mbili za mapumziko ya kitaifa ikiwemo siku ya kuaga wananchi wa dodoma na siku ya maziko ambayo ni tarehe 25 Machi. Wakati huo huo amewaomba raia wote kushirikiana na kuwa na utulivu wakati wa mazishi ambao unakuwa ni tofauti.
Katika hotuba yake hata hivyo ameonesha na kudhihirisha kwa taifa kuwa lina viongozi na katiba mambo ambayo ni muhimu kuliongoza nchi na kuwataka kila mmoja kuwa na matumaini na serikali iliyopo kwani amethibtisha wazi jinsi alivyo andaliwa vema na mtangulizi wake hayati Rais John Magufuli wakati akiwa ni makamu wake. Kwa maana hiyo Bi Suluhu amethibitisha kuendelea kuenzi yale yote ambayo mtangulizi wake amefanya na kwa kufanya hivyo ameomba kuwa ushirikiano na maombi kwa watanzania.
Katika hafla hiyo ya kuapishwa kwa rais viongozi mbalimbali wamehudhuria wakiwemo Marais wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliobaki na Zanzibar, Rais wa Zanzibar Hussein Mwinyi, spika wa Jamhuri wa muungano, Job Ndugai, jaji mkuu Profesa Ibrahim Juma pamoja na mawaziri mbalimbali na viongozi wa Kanisa. Kwa mujibu wa katiba ya Tanzania, Rais Samia Suluhu Hassan atatoa huduma yake kama rais kwa kipindi cha muhula wa urais hadi pale uchaguzi mwingine wa urais utakapofanyika.