Waziri mkuu wa Tanzania: Waliomung'unya fedha ya umma Mamlaka ya Bandari Tanzania, TPA, kukiona cha mtema kuni ikiwa kama watatiwa hatiani! Waziri mkuu wa Tanzania: Waliomung'unya fedha ya umma Mamlaka ya Bandari Tanzania, TPA, kukiona cha mtema kuni ikiwa kama watatiwa hatiani! 

Waliomung'unya Fedha ya Umma TPA, Kuchezeshwa "Mbegete"!

Waziri Mkuu amewasimamisha kazi Mkurugenzi wa Fedha wa TPA, Bibi Nuru Mhando pamoja na Meneja wa Matumizi ya Fedha wa TPA, Bibi Witness Mahela ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za matumizi mabaya ya fedha zinazowakabili. Waziri Mkuu amechukua hatua hiyo baada kupokea ripoti ya Ukaguzi Maalum uliofanywa na CAG katika hesabu ya Bandari ya Kigoma: 2017-2019 .

Na Ofisi ya Waziri Mkuu, - Dar es Salaam!

Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa amemuagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwenda kufanya ukaguzi maalum katika bandari za Dar es Salaam, Mwanza, Mtwara, Tanga na Kyela kutokana na kuwepo kwa matumizi mabaya ya fedha za umma. Pia Waziri Mkuu amewasimamisha kazi Mkurugenzi wa Fedha wa TPA, Bibi Nuru Mhando pamoja na Meneja wa Matumizi ya Fedha wa TPA, Bibi Witness Mahela ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za matumizi mabaya ya fedha zinazowakabili. Waziri Mkuu amechukua hatua hiyo baada kupokea ripoti ya Ukaguzi Maalum uliofanywa na CAG katika hesabu ya Bandari ya Kigoma kwa mwaka 2017/2018 na 2018/2019. Lengo la ukaguzi huo lilikuwa kujiridhisha kuhusu matumizi mabaya ya fedha za umma. Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo Jumapili, Desemba 27, 2020 katika kikao chake na Waziri na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Bodi ya Mamlaka ya Bandari Tanzania na Menejimenti ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) kilichofanyika katika ofisi za TPA jijini Dar es Salaam. Amesema taasisi hiyo imebeba taswira ya uchumi wa Taifa, lazima kazi ifanyike vizuri.

Mheshimiwa Majaliwa ameitaka Bodi ya Bandari Tanzania ihakikishe kwamba mamlaka hiyo inafanyakazi kwa weledi na isisite kuchukua hatua kwa mtumishi atakayebainika kutenda makosa na isimbebe kwa namna yoyote. Amesema miongoni mwa mambo yasiyoridhisha yanayofanywa na Mamlaka hiyo ambayo yanaikosesha Serikali mapato ni pamoja na msamaha wa kodi ya zaidi ya sh. bilioni mbili iliyoutoa kwa kiwanda cha saruji cha Mbeya licha ya kukataliwa na kamati ya misamaha.  Amesema licha ya kuongezeka kwa makusanyo lakini kati ya fedha inayokusanywa asilimia 70 tu ndiyo inayoongia Serikalini na kiasi kilichobaki kinaishia mifukoni jambo ambalo halikubaliki. ”Ripoti ya CAG ya Bandari ya Kigoma haijatufurahisha imeonesha mambo mengi mabovu.” Amesema katika hali isiyokuwa ya kawaida TPA iliidhinisha malipo ya sh. bilioni 8.2 kwenda Bandari ya Kigoma kwa ajili ya kwenda kufanya malipo mbalimbali huku ukomo wa bandari hiyo ni sh. bilioni 7.4.

Fedha hizo zilitumika kufanya malipo yasiyostahili kwa watu mbalimbali akiwemo mfanyabiashara wa duka la ujenzi mjini Kigoma Bw. Eliya Mtinyako aliyelipwa zaidi ya shilingi milioni 900. “Malipo haya yamefanyika huku kukiwa hakuna nyaraka zinazoonesha kama alilipwa kwa sababu zipi kwani mfanyabiashara huyo aliyelipwa hakuwahi kutoa huduma yoyote kwa mamlaka hiyo na wala si mzabuni. Pia amelipwa bila ya kuwepo kwa nyaraka za madai.”  Amesema licha ya upotevu huo wa fedha katika bandari hiyo ya Kigoma, pia Mhasibu wa Bandari ya Kigoma, Madaraka Madaraka alifuta madeni ya zaidi ya shilingi bilioni moja waliyokuwa wakidaiwa wateja bila ya kufuata taratibu na kuishababishia Serikali hasara. Kadhalika, Waziri Mkuu amesema ripoti hiyo ya CAG imebainisha uwepo wa malipo hewa ya zaidi ya shilingi bilioni mbili ambazo zimelipwa bila ya kufuata taratibu za malipo na wahasibu walipoulizwa walidai ni maelekezo kutoka makao makuu ya TPA.

Amesema walipofanya ukaguzi walibaini uwepo wa hundi 150 ambazo tayari zimesainiwa na wahusika wote na zimebaki wazi na mtu yeyote anaweza kujaza jambo ambalo ni kinyume na taratibu za Serikali kwani hazitakiwi kuwa hivyo. “Huu ni mpango wa wizi, Mamlaka kubwa kama hii hatuwezi kuacha hivi, hii fedha iliyopotea tungeweza kujenga zahanati, tungewapa TATURA wangejenga barabara nyingi tu. Mheshimiwa anapoelekeza fedha zipelekwe bandari ni kwa ajili ya kuboresha bandari yetu na lazima zitumike vizuri.” Kufuatia hatua hiyo, Waziri Mkuu amemuagiza DCI, Robert Boaz ahakikishe Mtinyako na Madaraka wanatafutwa popote walipo na kukamatwa. Pia ameagiza kwamba watumishi wote waliosimamishwa kazi wachunguzwe haraka na ikibainika kwamba hawana hatia warejeshwe kazi na wakikutwa na hatia hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.

Pia, Waziri Mkuu amemuagiza Mkurugenzi wa TAKUKURU afanye uchunguzi kuhusu Bw. Kalibilo ambaye ameonekana kuingiziwa kiasi kingi cha fedha bila ya kuwepo nyaraka zinazoonesha sababu za mtumishi huyo kulipwa fedha hizo. “Agosti anaonekana alilipwa shilingi milioni 55, Septemba shilingi milioni 53, Oktoba shilingi milioni 37 na Novemba shilingi milioni 19, lazima atafutwe popote alipo ijulikane fedha hizo alilipwa kwa ajili gani.” Hata hivyo, Waziri Mkuu amerudia agizo lake alilolitoa wiki iliyopita alipofanya ziara katika bandari ya Kagunga. Waziri Mkuu aliiagiza TPA ihakikishe kwamba ifikapo Januari Mosi, 2021 Bandari ya kimkakati ya Kagunga iliyoko katika Kata ya Kagunga wilayani Kigoma iwe imeanza kutoa huduma. Mradi wa ujenzi wa bandari ya kimkakati ya Kagunga ulikamilika 2017, ukihusisha ujenzi wa jengo la abiria pamoja na la mizigo, nyumba ya kuishi mtumishi na jengo maalumu lakini hakuna mtumishi katika bandari hiyo ambayo ujenzi wake uligharimu shilingi bilioni 3.8.

28 December 2020, 08:03