Mada ya Bayonuai kuzungumzwa katika Mkutano wa ngazi kuu ya UN
Mkutano wa ngazi ya juu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York Marekani tarehe 30 Sptemba umejikita na suala la bayonuai ambayo kwa muda sasa imekuwa ikiendelea kupotea na kuzusha hofu ya mustakbali wa viumbe vya dunia wakiwemo binadamu, mazingira na sayari yenyewe kwa kizazi hiki na vizazi vijavyo. Mada kuu inayojadiliwa katika mkutano huo uliowaleta pamoja nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kwamba wanapaswa kupiga hatua za haraka kuhusu bayoanuai kwa ajili ya maendeleo endelevu. Miongoni mwa wazungumzaji wakuu wa mjadala huo alikuwa ni Bi. Elizabeth Mrema katibu mtendaji wa mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya bayonuai.
Akizungumza na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa kabla ya kuwakilisha mada Bi Mrema ameelezea ni kwa nini suala hilo linapaswa kupewa uzito wa hali ya juu na hasa sasa kuliko wakati mwingine wowote. Bi Mrema emesema kuwa “Ni kweli kabisa kwamba binadamu wakati huu tumesimama njiapanda kuhusu urithi tunaowaachia vizazi vijavyo. Ushahidi wote wa kisayansi umeonyesha ukweli kwamba bayonuai inapungua kwa kiasi ambacho hakijapata kutokea na shinikizo zinazosababisha kupungua huku bado zinaendelea kuongezeka kwa mfano janga tulilonalo la COVID-19 limeangazia zaidi mahusiano kati yetu na maumbile au bayonuai.”
Bi Mrema akielezea athari zipi kubwa kama hatua hazitochukuliwa wakati huu Bi Mrema amesisitiza “Itapunguza uwezo wa bayonuai na mifumo ya ikolojia kutoa huduma muhimu za kuendeleza maisha, kuanzia usalama wa chakula, lishe kwa binadamu, ubora wa maji safi tunayopata kutoka kwa bayoanuai au hata magonjwa. Tumeingilia mapori nah ii imesababisha magonjwa kutoka kwa Wanyama kuja kwa binadamu, kutoka binadamu na kusambaa na kujikuta wote tumefungiwa kama ilivyo sasa hivi. Virusi, vijidudu kama vya corona vimeibuka kutokana na Wanyama wa porini”
Bi Mrema akiendelea kujibu swali ni kwa nini inakuwa ni vigumu kwa nchi kulizingatia hili na kulinda bayonuai kwamba, “Kwa kweli nchi nyingi na zote zinajitahidi sana , nafikiri kinachokosekana tunahitaji kupata kabisa utashi ule wa kisiasa toka kwa viongozi wetu wa juu kusaidia sekta zote zinazohusika moja, mbili bado nchi nyingi zinatoa ruzuku kubwa katika maeneo mengi ambayo hayasaidii bayoanuai zaidi yanaharibu bayonuai.”
Maoni yake kuhusu uhusiano gani uliopo baina ya maisha yetu ya kila siku na suala hili la bayonuai na maendeleo lakini pia katika kuhakikisha kwamba vizazi vijavyo havipotezi kila kitu Bi Mrema amejibu kuwa “Tutalaumiwa sana na vizazi vijavyo tusipoangalia, kulinda mazingira na kukomesha upotezaji wa bayonuai ni njia ya kufikia maendeleo endelevu. Kwa kulinda bayonuai tutachangia kufikia angalau malengo 11 kati ya 17 ya maendeleo endelevu”
Katika swali la nini wafanye wadau hawa wakubwa tuseme serikali, makampuni, sekta binafsi na watu binafsi ili kuhakikisha wanasaidia katika kuokoa bayoanauai, Bi mrema amejibu “Bayonuai sio sekta ya idara ya mazingira peke yake ni sekta zote katika serikali na watu wote mimi na wewe hata huko majumbani kila mtu anatakiwa kuzingatia na pia kuweza kuchangia katika kulinda bayoanuai.