Mali:Mapinduzi ya kijeshi kuelekea mabadiliko ya kiraia na uchaguzi!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Mkuu wa Majeshi nchini Mali Kanali Assimi Goita ambaye amepindua serikali na kulazimaisha Rais Boubakar Keita amehaidi kutenda mema katika serikali ya mpito kwa uchaguzi ulio huru. Na taarifa kwa msemaji wa wanajeshi wa waasi ameeleza kuwa wamechukua hatua hiyo ili kuiepusha Mali kutumbukia katika vurumai kubwa zaidi. Na kwamba sababu ya kuipindua serikali ni kurejesha utulivu na kusimamia kipindi cha mpito cha kuelekea kwenye uchaguzi katika muda utakaofaa. Hata hivyo hatua ya wanajeshi hao waasi imelaaniwa mara moja na viongozi wa kanda yote ya Sahel, Umoja wa Afrika, Umoja wa Ulaya na Umoja wa Mataifa.
Mgogoro unaanzia Kaskazini
Wanajeshi waliochukua madaraka nchini Mali kwa kushinikiza Rais Ibrahim Boubacar Keita ajiuzulu wametangaza kuunda “Kamati ya Kitaifa ya Wokovu wa Wananchi” kwa mujibu wa mahojiano na Vatican New na Padre Filippo Ivardi, mkurugenzi wa Gazeti la Nigrizia,na ambaye amechambua asili ya utata wa machafuko nchini humo. Kwa mujibu wa Padre Ivardi amebainisha kwamba katika kesi hiyo mgogoro umefunguliwa na ambao unatoka kaskazini mwa nchi hiyo, kesi inayounganishwa na kurudi polepole kutoka Libya kwa maaskari wa uhuru wa Tuareg ambao wamekuja mara baada ya kuanguka kwa serikali ya Ghaddafi. Katika hao wameongezeka vikundi vya kijihadi ambavyo vimeifanya eneo la kaskazini kuwa ukumbi wa mchezo mapambano magumu sana, ambapo vurugu za kijihadi zinaendelea hadi leo hii. Kutokana na kuongezeka hali ngumu sana ya maisha kwa idadi ya watu leo, inazidishwa hata kuathiriwa na Covid-19, wakati hali ya uchumi iko katika kuyumba yumba.
Masikitiko ya Ecowas
Naye Waziri wa mambo ya nje wa Niger iliyomo kwenye jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS Kalla Ankourao amesikitishwa na hatua iliyochukuliwa na wanajeshi wa Mali ya kumwangusha rais Keita. Ni kwa muda wa miezi miwili sasa walikuwa wakijaribu kusuluhisha na walitumaini kwamba watu wa Mali wangezifuata kanuni za jumuiya ya ECOWAS ambazo ni za demokrasia na utawala bora lakini kuangushwa serikali kumeyakomesha mazungumzo hayo kwa njia ya kikatili. Mwezi uliopita Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi iIlipendekeza kuundwa serikali ya umoja wa kitaifa na kuahidi kuendelea kumsaidia rais Keita, lakini pendekezo hilo lilitupiliwa mbali na wapinzani. Vile vile Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa litaitisha kikao cha dharura kuujadili mgogoro wa Mali. Ufaransa na Niger zimeomba kuitishwa kikao hicho. Mwanadiplomasi mmoja mwandamizi wa Umoja wa Mataifa ameliambia shirika la habari la AP kwamba kikao hicho kitakuwa cha faragha.