Watu wanazidi kuteseka nchini Burkina Faso na Kameruni!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Wakati janga la kibinadamu likishuhudiwa nchini Burkina Faso, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR limesema ongezeko katika mashambulizi linasababisha raia kukimbia kuelekea maeneo ya kusini karibu na Mali na Niger. Katika mji wa Kaya nchini Burkina Faso wakimbizi wanaendelea kukimbia wakati huu ambapo, UNHCR inasema wakimbizi 765,000 ni wakimbizi wa ndani. UNHCR imeweka makazi ya dharura kwa familia zilizo hatarini zaidi lakini kuna ukoseru wa maeneo salama zilizo na ulinzi huku wengi wa watu waliokimbilia kaya wakilala nje kwenye baridi.
Taarifa iliyotolewa hivi karibuni na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu masuala ya kibinadamu na msaada wa dharura OCHA, imenukuu ripoti za kuaminika zisemazo kuwa mnamo tarehe 14 Februari 2020 watu wenye kujihami kwa silaha waliwaua raia 20 wakiwemo watoto katika Kijiji cha Ntumbo, eneo la Kaskazini Magharibi mwa Cameroon. Takribani nyumba tisa ziliteketezwa kwa moto katika Kijiji na mashambulizi hayo yamesababisha watu 600 hadi 700 kutawanywa. Aidha taarifa ya OCHA imeeleza kuwa mnamo tarehe 16 Februari, kikosi cha msaada wa kibinadamu kilitumwa katika eneo ili kutathimini mahitaji ya wale waliotawanywa. Kutokana na hali mbaya ya usalama, kikosi hicho hakikuweza kufika katika Kijiji cha Ntumbo lakini maafisa waliweza kuzungumza na watu waliopoteza makazi na manusura walikuwa takribani kilomita mbili kutoka kijijini.
Katika maeneo ya Kaskazini Magharibi na Kusini Magharibi mwa Kameruni, raia wanabeba mzigo wa ghasia na wanaishi katika hofu. OCHA pia imesema kumekuwepo na ripoti za mara kwa mara kuhusu unyanyasaji unatekelezwa na pande zote ikiwemo mauaji, kulindwa kwa watekelezaji wa makossa hayo, utekaji, utesaji na watu kutendewa vibaya, kuteketezwa kwa nyumba na vijiji pamoja na kuvamiwa kwa shule na hospitali. Maafisa wa misaada pia wamekuwa wakitishiwa na kushambuliwa. “Kwa kurudia wito wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuwa, washambuliaji waache kufanya mashambulizi dhidi ya raia na waheshimu sheria za kimataifa za haki za binadamu.” Imesema OCHA
Jumla ya watu milioni 2.3 wako katika mahitaji makubwa ya chakula, malazi, vitu vingine ambavyo si chakula, pamoja na ulinzi, kwasababu ya mgogoro huo Kaskazini Magharibi na Kusini Magharibi mwa Kameruni. Idadi hiyo ya watu walioko katika mahitaji ni sawa na ongezeko la watu milioni moja ikilinganishwa na mwaka 2019.