Jeshi Iran limekiri kutungua kimakosa ndege ya abiria kuelekea Ukraine siku ya Jumatano 7 Januari 2020 na watu 176 waliokuwa kwenye ndege kupoteza maisha Jeshi Iran limekiri kutungua kimakosa ndege ya abiria kuelekea Ukraine siku ya Jumatano 7 Januari 2020 na watu 176 waliokuwa kwenye ndege kupoteza maisha  

Teheran:wanajeshi wa Iran wakiri kutungua Boeing 737 iliyowauwa watu 176!

Hatimaye Jeshi Iran limekiri kutungua kimakosa ndege ya abiria kuelekea Ukraine siku ya Jumatano 7 Januari 2020 kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na rais wa nchi.Watu 176 wametopeza maisha yao mara tu ndege kuanza safari yake kutoka uwanja wa Teheran.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Jeshi la Iran hatimaye limekiri kutungua kimakosa ndege ya abiria Ukraine siku ya Jumatano 7 Januari 2020. Aliyethibitisha taarifa hiyo ni rais wa Iran, Hassan Rohani, baada ya uchunguzi wa ndani uliofanywa na Nguvu za Kijeshi la Jamhuri ya kiislam. Taarifa ya jeshi inaeleza kuwa mkasa huo umetokana na makosa ya kibinadamu baada ndege hiyo kupita karibu na eneo nyeti linalomilikiwa na Kikosi cha Mapinduzi. Na Maafisa waliofanya kosa hilo wataadhibiwa, taarifa hiyo imeeleza.

Taarifa ya awali kukanusha

Iran awali ilikanusha vikali taarifa kuwa moja ya makombora yake yaliitungua ndege hiyo karibu na mji mkuu Tehran na wakati watu wote 176 ndani ya ndege hiyo wamepoteza maisha. Hata hivyo nchi hiyo ilikuwa tayari imesakamwa sana baada ya Marekani, Canada na Uingereza kudai kuwa taarifa za kijasusi walizonazo zinaonesha kuwa Iran iliidondosha ndege hiyo kwa bahati mbaya na moja ya makombora yake.

 Ndege ilianguka dakika chache kuondoka

Kuanguka kwa ndege hiyo kulitokea saa chache baada ya Iran kushambulia kambi za kijeshi za Marekani nchini Iraq kwa makombora ya masafa marefu. Vyombo vya habari vya Marekani vinadai kuwa Iran ilidhani kuwa ndege hiyo ilikuwa ya kivita ya Marekani, wakati taifa hilo lilipokuwa ikijiandaa kujibu mashambulio dhidi ya Marekani baada ya wao kushambulia vituo vyake vya kijeshi nchini Iraq kwa makombora. Iran ilirusha makombora kwenye kambi za Marekani Jumatano kama sehemu ya kisasi chake baada ya rais Donald Trump kuagiza shambulio la anga lililomuua Jenerali wa Iran Qasem Soleimani tarehe Januari 2020.

 Abiria waliuwa ni wa mataifa mbalimbali

Abiria waliokuwemo kwenye ndege hiyo ni raia 82 wa Wairan, 63 wa Canada, 11 wa Ukraine pamoja na wafanyakazi, Waswidi 10, raia wanne wa Afghanistan, watatu wa Uingereza na watatu wa Ujerumani,

Wito wa Papa Francisko

Ikiwa ni Dominika ya Pili ya kipindi cha Kuzaliwa kwa Bwana, tarehe 5 Januari 2020 mara baada ya sala ya Malaika wa Bwana Papa Francisko alitoa ushauri ili kuepusha kivuli cha uadui. Alisema: “katika sehemu mbalimbali za dunia inasikika hewa ya kutisha ya mivutano. Vita vinapelekea kifo tu na uharibifu.” Kutokana na hiyo anatoa wito kwa sehemu zote ili kubaki wamewasha mwanga wa majadiliano katika kujidhibiti na kuzuia kivuli cha uadui. Na alisema tuombe kwa kimya ili  Bwana atupe neema hii.

10 January 2020, 16:42