Siku ya ukoma duniani:usiwepo ukosefu wa haki,ubaguzi na ukoma ulimwenguni!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Ikiwa tarehe 26 Januari ni siku ya kimataifa ya ugonjwa wa ukoma, Papa Francisko amekumbusha pia kwamba:“leo inaadhimisha Siku ya ugonjwa wa Ukoma Ulimwenguni” Tuko karibu na watu wote walioathiriwa na dalili hizi za Hansen na wale wote kwa namna nyingine wanawasadia wagonjwa hao”. Mwaka huu umefikia toleo la 67 na ambalo linabeba kauli mbiu: Usiwepo kamwe ukosefu wa haki, ubaguzi, ukoma ulimwenguni.
Kufuatia na tukio hili hata mtaalamu huru wa Umoja wa Mataifa kuhusu kutokomeza ubaguzi dhidi wa watu walioathirika na ukoma, ametoa wito kwa serikali zote duniani kumaliza ubaguzi rasmi na usio rasmi dhidi ya maelfu ya wanawake na watoto walioathirika na ukoma.
Katika ripoti yake Bi Alice Cruz amesema: “Wanawake wengi na watoto walioathirika na ukoma ambao pia unafahamika kama ugonjwa wa Hansen ni waathirika wa unyanyapaa, unyanyasaji wa kimwili na kwa maneno, kucheleweshewa vipimo vya utambuzi na pia ukosefu wa uangalizi unaofaa.” Mtaalamu huyo wa Umoja wa Mataifa aidha ameelezea juu ya wasiwasi wake kuhusu “kutokuwepo kabisa mipango maalumu ya mataifa kushughulikia mahitaji fulani ya wanawake na watoto walioathirika na ukoma na pia kutokomeza ubaguzi na vurugu dhidi yao.”
Ripoti ya mwisho ya Bi Cruz imeeleza kuwa visa vingi vya wanawake na watoto walioathirika, vinapita tu bila kuripotiwa. Maelezo ya Bi Cruz yanasema kuwa ingawa mifumo ya kinga ya watoto inaonekana kuathiriwa zaidi na ukoma, asilimia 10 hadi 20 ya watoto wanaacha kutumia dawa kwa kuwa matibabu yaliyopo hayafai kwa umri wao. Zaidi ni kuwa wanawake walioathirika wanajikuta na msongo wa mawazo na hata mawazo ya kujiua hivyo mtaalamu huyo akatoa wito kwa serikali kote duniani kupata utatuzi kuhusu tatizo hili la ubaguzi