Mataifa husika heshimuni mikataba ya Vienna katika utendaji kazi
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Serikali ya Tanzania imewakumbusha na kuwataka mabalozi wanaoziwakilisha nchini zao nchini humo kufanya kazi zao kwa kuheshimu na kufuata mkataba wa Vienna na mikataba mingine ya Umoja wa Mataifa. Waziri wa mambo ya nje wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi amesema mabalozi hao wanapaswa kuzingatia hilo kwa vile mikataba hiyo ndiyo inayoangazia masuala ya kidiplomasia na yale yanayohusu mahusiano ya nchi moja na nyingine.
Wanadiplomasia wanapaswa kuendesha shughuli kwa kuzingatia miiko ya kimataifa
Akikutana nao kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa mwaka mpya, waziri Kabudi amewaambia wanadiplomasia hao kwamba wanapaswa kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia miiko ya kimataifa. Amesema shughuli zao za uwakilishi nchini zinapaswa kufanywa kwa kuzingatia miiko na desturi kama inavyoelezwa kwenye mkataba huo wa Vienna na mikataba mingine iliyoasisiwa na Umoja wa Mataifa.
Kwenda kinyume ni ukiukwaji wa taratibu za kidiplomasia
Amefahamisha kuwa kwenda kinyume na makubaliano yaliyoanishwa kwenye mikataba hiyo ni ukiukwaji wa taratibu za kidiplomasia jambo ambalo Tanzania haingependa kuona hilo. Kuhusu kile kinachoitwa mageuzi ya kiutendaji yanayoendelea kufanywa na serikali ya Tanzania, waziri Kabudi amedokeza kuwa wanadiplomasia hao wameonyesha utayari wa kuyaunga mkono wakipongeza eneo la kupambana na ufisadi na rushwa.
Prof. Kazungu:ni jambo la busara kufanya majadiliano hayo
Akizungumza baada ya kumalizika mkutano huo, Balozi wa Kenya nchini. Dan Kazungu ambaye pia ni Kiongozi wa Mabalozi wa Bara la Afrika amesema imekuwa jambo la busara kufanya majadiliano ya pamoja na serikali ya Tanzania hatua ambayo imetoa mwanga kwa wanadiplomasia hao kujua mengi yanayofanywa na serikali. Kauli ya Waziri Kabudi kuwataka wanadiplomasia hao kufungamana na mkataba wa Vienna, haijaashiria kulenga jambo lolote lililoibuliwa na mabalozi hao katika siku za hivi karibuni mbali ya kauli zilizowahi kutolewa na wanadiplomasia kadhaa wa nchi za magharibi wakikosoa kuhusu kuzorota kwa hali ya demokrasia na haki za binadamu.