Asilimia 20% ya vijana ulimwenguni kote wana shida za afya ya kiakili. Katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati karibu asilimia 15% wamefikiria kujiua. Asilimia 20% ya vijana ulimwenguni kote wana shida za afya ya kiakili. Katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati karibu asilimia 15% wamefikiria kujiua.  

UNICEF-WHO:Ongezeko la shida ya afya ya akili kwa watoto na vijana!

Asilimia 20% ya vijana ulimwenguni kote wana shida ya afya ya akili.Katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati karibu asilimia 15% wamefikiria kujiua.Hata hivyo kujiua ni sababu ya vifo vya vijana kuanzia umri wa miaka 15-19 duniani kote.Ni kwa mujibu wa Shirika la Watoto Duniani pamoja na Shirika la Afya Duniani wakijiandaa kufanya mkutano kuanzia 7-9-2019 Novemba,Firenze Italia.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Taarifa kutoka Shirika la  watoto UNICEF na Shirika la Afya duniani WHO wanasema kwamba  hadi asilimia 20% ya vijana ulimwenguni kote wana shida za afya ya akili na katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati,  karibu asilimia 15% wamefikiria kujiua. Hata hivyo kujiua ni sababu ya vifo vya vijana kuanzia umri wa miaka 15-19 duniani kote kwa mujibu wa maelezo hayo. Pamoja na viwango vya kutisha vya kujiumiza, kujiua na hisia mbaya kati ya watoto na vijana ulimwenguni kote, Shirika la watoto duniani (UNICEF) na Shirika la Afya Duniani WHO, zinashirikiana na baadhi ya wataalam ulimwenguni kukabiliana na  tishio hili linaloendelea.

Watoto na vijana wengi wana shida ya afya ya akili

Kwa mujibu wa Bi Henrietta Fore,Mkurugenzi mtendaji wa UNICEF amesema, watoto na vijana wengi, kutoka kila hali yote ya maisha na malezi, wana shida ya afya ya akili. Mgogoro huu ambao uko juu ya upeo, hauna kikomo  au mipaka. Na nusu ya shida ya afya ya akili inayoanza kabla ya umri wa miaka 14, wanahitaji mikakati ya haraka na ya ubunifu ili kuizuia, kuzitambua na inapobainika ni kuingilia kati kwa haraka iwezekanavyo, amesisitiza.

Mkutano wa UNICEF na WHO huko Firenze- Italia 7-9 Novemba

Katika juhudi za pamoja kwa ajili ya kukabiliana na shida za afya ya akili za watoto na vijana kwenye kilele cha ajenda ya afya duniani, UNICEF na WHO zitakuwa na mkutano kuhusu mada hiyo kuanzia tarehe 7 hadi 9  Novemba 2019 kwa mara ya kwanza huko Firenze nchini Italia.  Mkutano huo ni sehemu mpya ya moja ya mikutano duniani  ya mwaka ambayo inaongozwa na mada “Kuongoza akili”  ambapo UNICEF inakusudia kwa mara nyingine tena kuangazia shida kuu zinazoathiri watoto na vijana katika karne ya 21. Hata hivyo mkutano wa mwaka huu ni sehemu ya maadhimisho na mipango ya fursa ya maadhimisho ya miaka 30 ya Mkataba wa Haki za Mtoto na umeandaliwa kwa msaada wa kifedha wa Serikali ya Italia kupitia Ushirikiano wa Maendeleo ya Italia. Mkutano huo unakusudia kuunda safu za mapendekezo kutoka kwa wasomi, wanasayansi, serikali, wafadhili, biashara, mashirika ya kiraia na vijana ili kuchukua hatua madhubuti kuhusu dhalili hizo

Takwimu kuhusiana na matatizo ya akili. Shida siyo ya binafsi ni kijamii na kiuchumi

Kwa mujibu wa takwimu: hadi asilimia 20% za watoto duniani wanasumbuliwa na matatizo ya afya ya akili; hadi sasa vijana duniani kote wanashida ya afya ya kiakili; kujiua ni sababu ya pili kati ya vijana wenye umri wa miaka 15-19 duniani kote: karibu asilimia 15% ya vijana katika nchi zenye kipato cha chini na kati wanafikiria kijiua. Tatizo la  shida ya afya ya akili siyo ya kibinafsi, kwa maana ni ya kijamii na kiuchumi pia. Bado afya ya akili ya watoto na vijana mara nyingi imekuwa ikipuuzwa katika mipango ya afya kimataifa na kitaifa. Kuna watoto wachache sana ambao wanapata programu za kufundishia juu ya jinsi ya kudhibiti hisia ngumu. Amethibitisha hayo Dk. Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani. Na kuongeza kusema: "watoto wachache sana wenye shida ya afya ya akili wanapata huduma wanazohitaji na hivyo suala hili lazima ibadilike".

Mada nyingi za mkutano pia utazingatia mapungufu katika data 

Wakati wa mkutano wa unaohusu mada ya “kuongoza akili” 2019, rasilimali, ushirikiano, huduma, jitihada za kisiasa na msaada wa umma unaohitajika kukuza afya ya akili ya watoto na vijana vitachunguzwa. Aidha katika mkutano huo utachunguza misingi na matokeo kuanzia hali ya kisayansi na mazoezi, pamoja na maarifa ya hivi karibuni juu ya afya ya ubongo katika miaka ya kwanza ya maisha kama vile: wakati wa hatua ya kwanza ya utoto na ya pili na kuingia katika hatua ya ujana. Mkutano pia utazingatia mapungufu yaliyopo kwenye data ambazo zitahitaji kushughulikiwa, pia mipango ambayo imefanikiwa. Watachambua mkusanyiko wa magonjwa ya kiakili katika umri na eneo la kijiografia, sababu, vichocheo, mipango ya kuzuia na hatimaye kutibu shida na kukuza akili zenye afya.

06 November 2019, 13:58