Mabegi ya shule ya watoto  yametandazwa kama mfano wa makaburi kwenye viwanja vya makao makuu ya Umoja wa Mataifa, New York,Marekani kama ishara ya watoto waliokufa kwenye maeneo ya mizozo mwaka 2018. Mabegi ya shule ya watoto yametandazwa kama mfano wa makaburi kwenye viwanja vya makao makuu ya Umoja wa Mataifa, New York,Marekani kama ishara ya watoto waliokufa kwenye maeneo ya mizozo mwaka 2018. 

Watoto waathirika vitani hawatakaa darasani kutokana na sintofahamu za dunia!

Siku chache viongozi wa dunia watakusanyika kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kusherehekea miaka 30 tangu kupitishwa kwa mkataba wa kimataifa wa haki za mtoto,kwa njia hiyo UNICEF metandaza mabegi 3,758 ya watoto ikiwa ni ishara ya kukumbuka waathirika wa maelfu ya watoto katika nchi zenye migogoro na ambao mwaka huu hawataweza kukaa katika dawati la shule!Ni lazima yawakumbushe mkataba huo wa watoto kuwa uko hatarini.

Na Sr. Angela Rwezaula -Vatican

Kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa, jijini New York, Marekani, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF limetandaza mabegi 3,758 ya mgongoni yanayotumiwa na watoto wa shule kuonyesha madhara ya vita kwa watoto kwa mwaka 2018. Mabegi hayo yamepangwa kwa mfano wa makaburi ambapo kila begi moja linaashiria mtoto aliyepoteza  maisha kwenye maeneo yenye vita.

Taarifa ya UNICEF iliyotolewa jijini New York Marekani tarehe 8 Septemba 2019, imesema maonyesho hayo yatakuwepo hadi tarehe 10 mwezi Septemba 2019, kama ishara ya kutoa ujumbe kwa viongozi wa dunia maeneo mbalimbali ulimwenguni wakati huu ambapo watoto wanarejea shuleni siku chache kabla ya kuanza kwa mjadala wa ngazi ya juu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

UNICEF imesema pindi maonyesho hayo yatakapomalizika, mabegi hayo yatachukuliwa kuendeleza safari ya kusaidia elimu kwa watoto. Naye Bi Henrietta Fore, Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF amesema, “Mabegi ya mgongoni yanayotolewa na UNICEF kwa watoto yamekuwa kila wakati ishara ya matumaini na uwezo ambao mtoto anaweza kufikia pindi akipatiwa msaada,” .

Hata hivyo ni katika kuhimiza hilo wakati bado ni siku chache  viongozi wa dunia watakusanyika kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kusherehekea miaka 30 tangu kupitishwa kwa mkataba wa kimataifa wa haki za mtoto, CRC na hivyo maonyesho hayo ya mabegi ni lazima yawakumbushe kuwa mustakabali wa watoto uko hatarini.

12,000 walio uwawa au kujeruhiwa katika mapigano ya kivita: Kwa mujibu wa ripoti ya mwaka huu ya Umoja wa Mataifa, zaidi ya watoto 12,000 waliuawa au kulemazwa kwenye maeneo ya mizozo mwaka jana pekee wa 2018, na hivyo kufanya kuwa idadi kubwa zaidi tangu Umoja wa Mataifa uanze kufuatilia takwimu hizo. UNICEF imesema kwenye maeneo ya mizozo kama vile Afghanistan, Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, Somalia, Sudan Kusini, Syria na Yemen watoto wanalipa gharama kubwa ya vita.

10 September 2019, 15:34