Hija ya Papa Francisko nchini Madagascar: Wachimba madini wadogo wadogo na hali yao!
Na Padre Angelo Shikombe - Vatican
Wachimbaji wa Mgodi wa Akamasoa nchini Madagascar Jumapili ya tarehe 8 Septemba 2019, wameungana na wachimbaji wengine nchini humo, kumkaribisha na kumwombea Baba Mtakatifu Francisko neema na baraka za Mwenyezi mungu na kutoa ushuhuda wa maisha yao ya kiimani. Katika kushuhudia imani iliyo hai mbele za Mungu, wameeleza jinsi Mungu anavyowasaidia kuvuka changamoto mbalimbali ya mazingira magumu ya kazi zao, na kutoa ushuhuda wa imani yao kwa Mwenyezi Mungu, inayopenya ugumu wa changamoto na matatizo makubwa wanayowakabiliana nayo katika shughuli zao za kila siku. Tumaini hili linalojifunua kwa njia ya furaha kubwa waliyonayo inayotirirka katika mioyo yao inayofumbatwa katika bidii yao kubwa ya kufanya kazi ngumu na halali na zenye kipato kidogo.
Aidha wakielezea ugumu wa mazingira ya uchimabji na changamoto nyingine nyingi wanazokumbana nazo, Mwakilishi wa wachimbaji hao ameshuhudia kuwa, wachimbaji wamebaki na imani kubwa kwa Mwenyezi Mungu ambaye ndiye mgawaji wa riziki zote. Wakieleza hisia zao mbele ya Baba Mtakatifu, wachimbaji hao wamesema, wameupasua mwamba kwa 30% kwa kutumia nguvu zao ili waweze kujipatia mahitaji yao ya kila siku. Hata hivyo walimweleza Baba Mtakatifu kuwa, kipato chao bado ni cha hali ya chini ukilinganisha na kazi wanazozifanya. Wanaipokea hali hiyo duni kwa furaha kubwa kwa sababu ni wanasehemu ya kujipatia riziki yao halali.
Hivyo wachimbaji hao wamekiri waziwazi kuwa, hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Madagascar imekuwa chanzo cha furaha na tumaini kuu, inayowaimarisha na kuwaongezea bidii katika kutimiza wajibu wao katika familia zao. Aidha, Wachimabji hao wamemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kutetea haki za wafanyakazi ulimwenguni kote, jambo linaloonesha kumtetea mnyonge dhidi ya udhalimu wa wenye madaraka na wenye nguvu za kifedha. Kwa niaba ya wafanyakazi wote wa Mgodi wa Akamasoa, mwakilishi wa wachimbaji waliweza kutoa ushuhuda wa kazi njema wanazozifanya ili kutegemeza Kanisa, zikiwemo kutoa zawadi kwa ajili ya Kanisa kuu lililoko umbali wa mita 50 kutoka mgodi wa Akamasoa.
Ushuhuda wa kiimani Mgodini Akamasoa: Wakielezea hali yao ya imani kwa Mwenyezi Mungu, wachimbaji wa mgodi wa Akamasoa wameshuhudia kuwa, wamechimba shimo mlimani ambamo ndani yake kuna Altare wanazotumia kusali, kumwabudu Mungu na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuadhimisha sadaka ya Ekaristi Takatifu katika ibada ya Misa Takatifu hususani mara tatu kwa Mwaka yaani; katika sherehe ya kupaa Bwana Mbinguni, sherehe ya kupalizwa Bikira Maria Mbinguni na sherehe ya Watakatifu wote.