Moja ya kijiji nchini Burkina Faso Moja ya kijiji nchini Burkina Faso 

Burkina Faso:Umoja na Mshikamano unahitajika ili kushinda itakadi kali za kidini!

Mashambulizi ya kigaidi yanazidi kuongezeka na kuwauwa mapadre,kutekwa nyara wakristo na wakati huo huo hata makanisa kuharibiwa na kuchomwa moto.Kesi hii imejitokeza nchini Burkina Faso wakati wa kuadhimisha misa Takatifu Tarehe 12 Mei 2019.

Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican

Kanisa na watu wote nchini Burkina Faso wanajikuta katika mantiki ngumu ya mateso ya kiajabu! Mashambulizi ya kigaidi yanazidi kuongezeka na kuwauwa mapadre, kutekwa nyara wakristo na wakati huo huo hata makanisa kuharibiwa na kuchomwa moto. Katika mantiki hii ya vurugu na kutumia nguvu na mateso, ndiyo itaangazwa zaidi na  Baraza la Maaskofu katoliki kitaifa na  Eneo Afrika Magharibu kwa pamoja (RECOWA-CERAO ) ambao wameanza mkutano wao kuanzia tarehe 13 hadi 20 Mei huko Ouagadougou, ikiwa ni kwa mara ya tatu wanafanya  Mkutano wao Mkuu wa mwaka pamoja

Wakristo nchini Burkina Faso, kama wengine wengi barani Afrika, wanasumbuliwa na vurugu na nguvu zinazo sababishwa na kukiri imani yao. Kwa maana hiyo mantiki ya mateso itaweza kuzungumzwa kwa kina na  Maaskofu hao  ili waweze kupeleka roho ya kinabii na kidugu kwa msaada wao wa kimadili na kiroho  na zaidi  kwa wakristo kwa namna ya pekee  watu wa Burkina Faso kwa ujumla. Katika Bara la Afrika wanasema mara nyingi kuna hali ngumu ya umasikini japokuwa ni bara ambalo limejulikana  kuwa na urafiki wa kweli. Japokuwa  kwa bahati mbaya inakuja kwa mara nyingine tena suala la kutumia jina la Allah na kuwaua watu!

Padre  Siméon Yampa kuwawa na waamini wengine wakati wa maadhimisho ya misa

Haya ni mawazo ya Padre Donald Zagore wa  Shirika la Kitume la Afrika  (SMA) akifafanu tafakari yake katika Shirika la habari za Kimisionari Fides, mara baada ya tukio  baya ya mashambulizi ya kigaidi huko Burkina Faso, mahali ambapo, magaidi walivamia Kanisa na kumuua Padre Siméon Yampa akiwa anaadhimisha Misa Takatifu, Jumapili 12 Mei 2019 pia waamini wengine watano na  kabla ya kukimbia  waliacha wameteketeza moto Kanisa, pamoja na majengo mengine kama vile  maduka likiwemo hata  kituo cha afya.

Padre  Siméon Yampa alizaliwa kunako tarehe 19 Februari  1985. Na alikuwa amepata daraja takatifu la upadre kunako Julai  2014 jimbo Katoliki la  Kaya. Na kwa mujibu wa Askofu wa jimbo lake Théophile Nare, amethibitisha katika vyombo vya habari Fides kuwa, Padre huyo alikuwa ni mtu mtiifu, mnyenyekevu na alijazwa upendo na kupenda wana parokia hadi kutoa sadaka ya maisha yake. Kutokana na mauaji hayo, Padre Donald Zagore anasema, ukweli ni kwamba Allah hawezi katu kutuma mtu yoyote kwenda kuua kwa niaba yake. Wale wote ambao wanaua watu wakati wakitamka jina la Allah ni wahalifu na ambao wanastahili kukamatwa na kuhukumiwa kwa mujibu wa sheria.

Leo hii na zaidi katika Kanisa la Afrika Magharibi, kwa njia ya Maaskofu wanataka kuonesha duniani kote kuwa, wakristo wa Burkina Faso, hawako peke yao katika mapambano dhidi ya ugaidi wa kidini. Mapambano hayo yatashinda kwa sababu ya utambuzi kuwa, ubaya kwa kawaida siyo neno la mwisho wa  maisha na kutokana na hiyo inawezekana kupambana dhidi ya changamoto hizi mbaya kama serikali zitajihusisha kwa namna ya dhati na  kwa mwafaka. Padre Zagore anahitimisha kwa kusema ni kipindi sasa hata serikali  kuanza kuungana kwa dhati kutumia zana zote za lazima ili kuweza kufikia mwisho wa majanga haya dhidi ya ubinadamu. Katika umoja na mshikamano tunaweze kweli kushinda itikadi kali na mbaya za kidini.

Umoja wa Mataifa walaani mashambulizi ya kigaidi huko Burkina Faso

Umoja wa Mataifa umelaani vikali shambulio lililofanyika tarehe 12 Meo 2019  kwenye Kanisa Katoliki Kaskazini nchini Burkina Faso ambalo limekatili maisha ya watu sita. Katika ujumbe wake kupitia ukurasa wake wa twitter Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Maria Espinosa, ametoa wito wa wauaji kuwajibishwa. “Hatuwezi kuvumilia chuki. Haki ya msingi ya uhuru wa dini ni lazima iheshimiwe kila mahali.” Naye Metsi Makhetha, mratibu mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Burkina Faso, ametoa ujumbe kupitia twitter yake pia akilaani vikali mashambulizi ya leo Dablo, ambapo ameyaita kuwa ni ya kikatili huku akitoa salamu za rambi rambi kwa familia za waathirika na walio poteza maisha.

Shambulio hilo la risasi limekuja siku chache baada ya tahadhali kutolewa na maafisa wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa akiwemo Bi. Makhetha “kuhusu hali isiyo ya kawaida ya kuongezeka kwa mashambulizi ya silaha  huko Sahel ambayo yanaweka mustakabali wa kizazi chote katika hatari kubwa. “ Machafuko yanasambaa Mali na Niger, lakini pia Burkina Faso na kuna hatari kubwa ya kusambaa katika mataifa mengine ya Afrika Magharibi. Machafuko haya ya karibuni yamesababisha ongezeko la ⅕ ya watu wanaotawanywa nchini humo na katika miezi 12 iliyopita na  kumeshuhudiwa zaidi ya watu 330,000 walioamua kufunga virago na kukimbia mbali ya wakimbizi 100,000.

Kwa mujibu wa Bi. Makhetha kundi lenye silaha lililohamasishwa na ISIS linatishia kuvuruga amani na utamaduni wa muda mrefu wa suluhu ya migogoro ya kijamii. Kwa mana hiyo: “Umoja wa Mataifa, mashirika wadau wa kibinadamu na serikali za ukanda huo wameongeza juhudi  za operesheni zao lakini ni lazima tuongeze bidii.”

13 May 2019, 15:45