WHO:Huduma kwa ajili ya Ebola nchini DRC yarejeshwa tena!
Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Shirika la afya ulimwenguni, (WHO) limesema kuwa operesheni za kukabiliana na mlipuko wa ebola kwenye jimbo la Kivu Kaskazini, nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo, DRC zimeanza tena baada ya kusitishwa kwa muda. Hata hivyo tahadhali katika maeneo yote yaliyo na mlipuko wa ugonjwa huo wa hatari imesisistizwa kwa ajili ya wema wa afya ya wote.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) operesheni za kukabiliana na gonjwa hilo zilikuwa zimeathiriwa na mzozo katika mji wa Beni ambao ni kitovu cha mlipuko wa ebola mwishoni mwa mwezi Desemba mwaka jana. Shirika la Afya Ulimwenguni aidha limesema kufuatia uongozi kutoka kwa serikali na ushirikiano na wadau, operesheni za kukabiliana na ebola zimerejea katika vituo vyote lakini imetoa tahadhari kuwa iwapo kutakuwa na usumbufu wowote huenda ukaathiri hatua zilizopigwa kama kutashuhudiwa vipindi virefu vya ukosefu wa usalama.
Shirika hilo la afya limetaja changamoto kubwa ya harakati za kukabiliana na Ebola kuwa ni hali ya usalama, kutoaminiana kwa baadhi ya watu walioathirika na mbinu dhaifu za kuzuia na kudhibiti ebola katika vituo vingi vya umma na binafsi vya afya. Kufikia sasa visa 625 vimeripotiwa ambapo visa 577 vimethibitishwa na vifo 377 vimeandikishwa tangu mlipuko ulipotangazwa Agosti mwaka jana 2018. Shirika la afya ulimwenguni, inaripoti kuwa zaidi ya watu 56,500 wamepatiwa chanjo dhidi ya ebola, na watu 220 wamepona.