Tarehe 19 Novemba ya kila mwaka ni Siku ya Kimataifa ya ajali barabarani Tarehe 19 Novemba ya kila mwaka ni Siku ya Kimataifa ya ajali barabarani 

WHO:kila siku wanakufa watu 3,400 kutokana na ajali barabarani

Kila siku ajali za barabarani hukatili uhai wa maelfu ya watu, wakati huo kuwaacha wengine na ulemavu wa maisha na kuathiri mfumo mzima wa familia nyingi duniani. Na watu 3,400 hufa kila siku kutikana na hajali hizo, kwa mujibu wa Shirika la Afya katika Siku ya Kimataifa ya Ajali barabarani inayokumbukwa kila tarehe 19 Novemba ya kila mwaka

Sr. Angela Rwezaula - Vatican

Kutokana na hilio Shirika la afya duniani, (WHO) limesema ni wakati wa kuchukua hatua dhidi ya tatizo hili sasa. Katika taarifa iliyotolewa siku ya kuwakumbuka waathirika wa ajali za barabarani tarehe 19 Novemba , Shirika la Afya  limesema maisha ya watu milioni 5 yanaweza kuokolewa katika muongo wa “Hatua kwa ajili ya usalama barabarani ulioanza 2011-2020” ambapo wanasisitiza  kuwa lengo ni kupunguza kwa asilimia 50 majeruhi na vifo vitokanavyo na ajali za barabarani ifikapo 2020 ,  katika juhudi za kutimiza malengo ya maendeleo endelevu au SDG’s hususani lengo la afya namba 3.6.

Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani ni watu 3,400 hupoteza maisha kila siku kutokana na ajali za barabarani na athari zake kwa familia na jamii kwa ujumla ni kubwa sana, kwani vifo hivyo vya ghafla huacha kovu la milele kwa familia ikiwa ni pamoja na kwa majeruhi katika kila kona ya dunia na huongeza idadi ya mamilioni wanaosalia kuwa tegemezi kwa njia moja au nyingine.

Siku hii pia inalenga kushikamana na mamilioni ya waathirika kote duniani ambao wanataka kutambulika na watu kufahamu madhila yanayowakabili kutokana na ajali hizo. Utafiti wa WHO unaonyesha kuwa asilimia 40-50 ya madereva huendesha kasi zaidi ya kipimo kinachonatakiwa, hali ambayo husababisha ajali moja kati ya tatu zinazotokea barabarani kila siku.

Kwa kutambua umuhimu wa kupunguza ajali hizo, mwezi Aprili mwaka huu Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliamua kupitisha hatua kadhaa ili kuchapusha mchakato wa kufikia malengo ya SDG’s yanayohusiana na usalama barabarani. Miongoni mwa hatua hizo ni kukubali pendekezo la serikali ya Sweden kuwa mwenyeji wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa ngazi ya juu kuhusu usalama barabarani utakaofanyika 2020, pia makubaliano ya malengo 12 ya kimataifa ya usalama barabarani na kuanzisha wakfu wa Umoja wa Mataifa wa usalama barabarani.

Siku ya kuwakumbuka waathirika wa ajali za barabarani duniani huadhimishwa kila mwaka katika Jumapili ya tatu ya mwezi Novemba kwa ajili ya kuwaenzi mamilioni ya watu waliopoteza maisha na kujeruhiwa katika ajali za barabarani duniani pamoja na familia zao, marafiki na wengine wengi walioathirika kwa njia moja au nyingine kutokana na ajali hizo.

Siku ya Kimataifa ya ajali barabarani
20 November 2018, 15:48