Tafuta

Ibara ya 17 ya haki za binadamu inazungumzia haki ya mtu kumiliki mali yeye mwenyewe au ushirika na mtu mwingine, lakini, wanawake wajane au wenye talaka hawawezi faidika,nchi za Afrika Ibara ya 17 ya haki za binadamu inazungumzia haki ya mtu kumiliki mali yeye mwenyewe au ushirika na mtu mwingine, lakini, wanawake wajane au wenye talaka hawawezi faidika,nchi za Afrika 

Moja ya Ibara 30 za haki za binadamu ni haki ya kumiliki mali!

Tunapokaribia kilele cha kutimia kwa miaka 70 tangu tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa lililowekwa kunako tarehe 10 Desemba 1948, bado inaonesha ni jinsi gani tamko hilo ni ndoto kufikia malengo yake duniani kote, kati ya Ibara 30 za Tamko hilo

Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa mwaka huu 2018 linatimiza miaka 70, kwani lilitangazwa kunako tarehe 10 Desemba 1948. Tamko hilo lina ibara 30 ambapo leo tutazame katika ibara ya 17 inayozungumzia haki ya mtu kumiliki mali yeye mwenyewe au kwa ushirika na mtu mwingine au wengine. Ibara hii inazingatia ukweli kwamba baadhi ya watu wananyimwa haki hiyo kwa misingi mbalimbali ikiwemo rangi, jinsia, kabila, dini au umri.

Ibara ya 17 pia inahusu mtu asinyangangwe mali yake bila sheria

Miongoni mwa mali zinazotajwa katika Ibara ya 17 ni pamoja na kiwanja au ardhi ikimaanisha kuwa mtu yeyote ana haki ya kumiliki ardhi, ali mradi azingatie sheria. Hata hivyo katika jamii nyingi ikiwemo barani Afrika, umiliki wa ardhi umekuwa na changamoto kubwa hususan kwa wanawake na wasichana. Mfano tu ni nchini Ethiopia ambako ilikuwa ni shida ambapo raia wengi wa kawaida walipoteza mali kwa mfano viwanja  kutokana na  kutokuwa na ushahidi. Mfano ikiwa wanamiliki viwanja lakini hawana hati ya umiliki ndipo serikali ikafanya mikakati ya  kuwaondolea adha hiyo kwa kuwapatia hati. Mmoja  waLE walionufaika ni mkulima mmoja kwa jina Melkam Amogne aliyepambana mpaka alipopatiwa  hati ya umiliki na akapata kupumua na kwa  sasa anathibitisha kwamba  “sasa ikiwa mtu yeyote atajaribu kuninyanganya ardhi yangu ninaweza kumshataki”. Lakini hiyo ni moja wa dhirisho la ibara hiyo ya 17 ya tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa.

Jamii nyingi zinabagua watu wa jinsia ya kike kwa mfano walio na talaka au wajane

Jamii zingine huwa zinawabagua watu wa jinsia ya kike hususan ikiwa wanawake wamepewa talaka au wamebaki wajane. Familia za wanaume hufanya kila juhudi kuwanyang’anya ardhi hiyo licha ya mwanamke huyo kuwa na watoto, na kesi ni nyingi sana kwa upande wa Afrika. Tukibaki katika nchi ya Ethiopia pia ndiyo itakuwa mfano mwingine. Katika kutilia mkazo wa ibara ya 17 ya tamko la haki za binadamu, pia sehemu nyingine ya ibara hiyo inasema kuwa, “ Mtu asinyanganywe mali yake  bila sheria”. Lakini mama mmoja wa watoto watano mwenye umri wa miaka miaka 45 yalimpata yaliyo mazito. Mmoja wa watoto wake, Mengaw Simachew anmeeleza magumu ya mama yake  aliyopitia kuweza kupata uhakika wa kumiliki mali yake yaani kipande cha ardhi. Amesema: “Kabla ya hati ya kumiliki kutolewa kulikuwa na mivutano ya mipaka ya ardhi hiyo na watu wakiwa wanachukua  kwa nguvu ardhi ambayo haikuwa ya kwao.”  Naye mjane Nitsu Simachew  akidhibitisha hilo, anasema kuwa:  anafurahi kupata hati inayoonyesha kama ndiye mmilikaji halali wa kipande hicho cha ardhi, na kuifanya  haki itendeke na kwenda sambamba  na ibara ya 17 inayosema kuwa, kila mtu ana haki ya kumiliki mali.

Miaka 70 ya tamko la haki za binadamu duniani, haijawa tiketi kwa kila mtu kufarahia haki msingi

Katika mifano hiyo midogo kati ya mifano mimgi iliyopo duniani, ndipo unaweza kuthibitisha kwa yale aliyotamka Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kwamba: miaka 70 ya tamko la haki za binadamu duniani, haijawa tiketi kwa kila mtu kufarahia haki za msingi zilizoainishwa katika nyaraka hiyo. Aliyatoa kauli hiyo kunako tarehe 26 Septemba 2018 jijini New York, Marekani kwenye kikao cha ngazi ya juu kuhusu miaka 70 ya nyaraka hiyo na nafasi yake katika kuchagiza malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.

Akiendeleza kusisitiza alisema: “Haki zilizotajwa katika nyaraka hizi ya msingi ni haki za kila mtu, popote alipo na hazina mpaka wowote ule iwe ni ule unaoonekana au wa kimaadili. Haki hizi hazibanwi na utaifa, mazingira, jinsia, rangi, dini au imani,”. Wakati huo huo aliweza kunukuu hata  ibara ya kwanza ya tamko hilo inayosema kuwa binadamu wote wanazaliwa wakiwa huru na sawa kiutu na kihaki. Akisistiza zaidi alionesha kusikitika kwamba, bado safari ni ndefu ili haki hizo ziweze kufurahiwa na watu wote duniani kote!

Watu wengi duniani bado wanakumbwa na shida kutokana na haki zao kukiukwa

Ukosefu wa usawa wa kijinsia ni moja ya changamoto kubwa zinazokabili haki za binadamu, kwani Bwana Guterres alikumbuka  pia makundi ya wakimbizi na makabila madogo madogo kwamba, mara kwa mara wananyimwa haki zao. Hata hivyo kulingana na mantiki hizo alitoa hata wito kwa nchi ambazo bado hazijatia saini au kuridhia makubaliano mawili ya haki za binadamu ikiwemo lile la haki za kisiasa na mkataba wa kimataifa wa haki za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni zifanye hivyo haraka iwezekanavyo. Alitumia fursa hiyo pia kukumbusha vijana kuwa wao ndio wahifadhi wa kweli wa tamko la haki za binadamu hivyo aliwasihi wasonge mbele na kuhoji jinsi ambavyo Umoja wa Mataifa na wanachama wanachukua hatua kwa ajili ya maslahi na haki za binadamu.

TAMKO LA HAKI ZA BINADAMU

 

 

27 November 2018, 11:08