Ripoti ya FAO inasema, mtu mmoja kati ya 9 duniani ana njaa!
Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Ripoti mpya ya Umoja wa Mataifa inaonesha kuwa idadi ya watu wenye njaa inaongezeka na milioni 821 ilikuwa mwaka jana, ikiwa ni sawa na mtu mmoja kati ya watu 9.
Ripoti hiyo iliyozinduliwa tarehe 11 Septemba 2018 mjini Roma, Italia ni ya mashirika matano ya Umoja wa Mataifa ikiwemo la chakula na kilimo FAO, mfuko wa kimataifa wa maendeleo ya kilimo, IFAD, mpango wa chakula duniani, WFP, lile la kuhudumia watoto, UNICEF pamoja na la afya, WHO.
Ripoti inasema hatua ndogo zimepigwa katika kushughulikia aina mbalimbali za utapiamlo kuanzia udumavu wa watoto hadi utipwatipwa wa watu wazima, na hivyo kuhatarisha afya za mamilioni kadhaa ya watu. Hali ni mbaya katika maeneo ya Amerika ya kusini na maeneo mengi ya Afrika ilhali mwelekeo wa kukabiliana na lishe isiyo ya kutosha kwa nchi za Asia ukionekana kusuasua.
Ripoti imetaja chanzo kuwa, ni mabadiliko ya tabianchi unaoathiri mwelekeo wa mvua na misimu ya kilimo ikitaja pia hali za kubadilikwa kwa hewa kama vile ukame na mafuriko kuwa vichochezi vya ongezeko la njaa, bila kusahau mizozo na kudorora kwa uchumi.
Naye Mkurugenzi Mkuu msaidizi wa FAO Kostas Stamoulis ametaja kinacho shangaza zaidi kwamba “Suala la ukosefu wa damu pia limetajwa likiathiri zaidi wanawake wenye umri wa kubeba ujauzito na kuzaa watoto, ambapo ripoti imesema linaweza kuwa na athari kubwa zaidi kwa afya siyo tu ya mama anapojifungua bali pia kwa mtoto anayezaliwa."
Hata hivyo Bwana Stamoulis amesema kuwa licha ya hali hiyo kuna matumaini kwa maana anasema “Lazima tuwe na matumaini. Lakini matumaini haya haimaanishi kuwa tuakae tu. Ninaamini kuwa lengo la kutokomeza njaa ifikapo mwaka wa 2013 bado linaweza kufikiwa kwa kuwa tuna tekenolojia, elimu na maarifa na tuna uelewa wa jinsi ya kufanya.