Tafuta

Kanisa la Tanzania linampata Askofu Mpya wa Jimbo la Iringa. Kanisa la Tanzania linampata Askofu Mpya wa Jimbo la Iringa. 

Papa Francisko amemteua Pd.Romanus Elamu Mihali kuwa Askofu mpya wa Iringa

Papa Francisko ameridhia maombi ya kung'atuka kutoka shughuli za kichungaji za Jimbo Katoliki la Iringa nchini Tanzania,yaliyowakilishwa na Askofu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa na wakati huo huo akamteua Padre Romanus Elamu Mihali kuwa Askofu Mpya wa Jimbo hilo.Hadi uteuzi huo alikuwa makamu Askofu wa Mafinga.

Na Angella Rwezaula – Vatican.

Jumanne tarehe 28 Januari 2025, Baba Mtakatifu Francisko amepokea barua ya maombi ya kung’atuka kutoka katika  shughuli za kichungaji kwa ajili ya Jimbo Katoliki la Iringa nchini Tanzania yaliyowakilishwa na Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa baada ya kufikisha umri wake wa kustaafu, na wakati huo huo, Baba Mtakatifu akamteua Askofu Mpya wa Jimbo hilo Mhes, Padre  Romanus Elamu Mihali,  wa jimbo la Mafinga ambaye hadi uteuzi wake alikuwa  Makamu Askofu wa Jimbo la Mafinga na Paroko wa Ujewa.

Wasifu

Padre Mihali alizaliwa tarehe 10 Juni 1969 huko  Itulituli, Wilaya ya Mufindi, Mkoa wa Iringa. Mara baada ya majiundo yake ya Falasafa na Taalimungu katika Seminari Kuu ya Songea,  alipewa daraja  takatifu la  Upadre kunako tarehe 13 Julai 2000 kwa ajili ya jimbo la Iringa.

Nyadhifa

Ameshikilia nyadhifa mbali mbali na kuendelea na masomo zaidi kama:  Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu Paulo Mtume huko Ilula, Iringa (2000-2003); Mlezi na Mkufunzi wa Seminari Ndogo ya Mtakatifu Kizito, Mafinga(2003-2005); Masomo ya Uzamili wa Sayansi katika Sayansi ya fani ya wanyama na kupata  Shahada yake  katika Chuo Kikuu cha Kerala nchini India (2005-2011); Paroko Msaidizi wa Bikira Maria wa Fatima huko  Usomaki, Iringa (2012-2015); Paroko wa Parokia ya Bikira Maria Mpalizwa, Ujewa  Iringa (2015-2024).

Baada ya kusimikwa jimbo la Mafinga  kunako 2024 kwa kupata hata Askofu mpya wa Jimbo hilo, Padre Romanus alipewa nafasi ya kuwa Makamu Askofu wa Jimbo hilo la Mafinga na Paroko wa Parokia ya  Bikira Maria Mpalizwa (Mafinga) hadi uteuzi huu.

Askofu Mstaafu wa Iringa
Askofu Mstaafu wa Iringa

Askofu Mstaafu Tarcisius Ngalalekumtwa ataendelea kuwa Msimamizi wa Kitume wa Jimbo la Iringa hadi Askofu  pale Askofu Mteule atakapowekwa wakfu wa kiaskofu kwa ajili ya jimbo hilo hilo.

Askofu Mpya wa Irainga
28 Januari 2025, 18:09