Tafuta

Askofu mkuu  Hon Tai-Fai, SDB. Balozi mpya wa Vatican nchini Libya, 2023. Askofu mkuu Hon Tai-Fai, SDB. Balozi mpya wa Vatican nchini Libya, 2023. 

Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai, S.D.B. Balozi mpya wa Vatican Nchini Libya

Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai, S.D.B., alizaliwa 1950 huko mjini Hong Kong. Tarehe 15 Agosti 1975 akaweka nadhiri za daima na hatimaye akapewa daraja Takatifu ya Upadre, tarehe 17 Julai 1982. Kunako tarehe 23 Desemba 2010, Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI akamteuwa kuwa Askofu mkuu na Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu na kuwekwa wakfu kama Askofu mkuu tarehe 5 Februari 2011. Amewahi kuwa Balozi: Ugiriki na Malta.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai, S.D.B., kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Libya na kabla ya uteuzi huu, Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai alikuwa ni Balozi wa Vatican nchini Malta na amewahi pia kuwa Balozi wa Vatican nchini Ugiriki. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai alishawahi kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu. Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai, S.D.B., alizaliwa tarehe 21 Oktoba 1950 huko mjini Hong Kong. Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa katika Shirika la Wasalesian wa Don Bosco, tarehe 15 Agosti 1975 akaweka nadhiri za daima na hatimaye akapewa daraja Takatifu ya Upadre, tarehe 17 Julai 1982. Kunako tarehe 23 Desemba 2010, Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI akamteuwa kuwa Askofu mkuu na Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu na kuwekwa wakfu kama Askofu mkuu tarehe 5 Februari 2011. Tarehe 6 Juni 2016 akateuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Msimamizi wa Kitume wa Jimbo kuu la Agaña, Guam lililoko kwenye Bahari ya Pacific kuanzia tarehe 6 Juni 2016 hadi 31 Oktoba 2016. Tarehe 28 Septemba 2017, Baba Mtakatifu akamteuwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Ugiriki. Tarehe 24 Oktoba 2022, akateuliwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Malta. Na tarehe 18 Mei 2023, Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai, S.D.B., kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Libya. Askofu mkuu Savio Hon Tai-Fai, S.D.B., ni kati ya “vigogo” waliojisadaka kutafsiri Katekisimu ya Kanisa Katoliki katika lugha ya Kichina; amana, urithi na utajiri wa imani; matunda ya Maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na chombo cha kusaidia mchakato wa ukuaji na ushuhuda wa imani kwa Kristo Yesu na Kanisa lake ambayo kwa Mwaka 2022, Mama Kanisa alifanya kumbukizi ya miaka 30 tangu kuidhinishwa kwake. 

Libya: Changamoto ya ulinzi, usalama na wakimbizi
Libya: Changamoto ya ulinzi, usalama na wakimbizi

Katekesimu ya Kanisa Katoliki ni chachu ya utakatifu wa maisha yenye mvuto na mashiko katika azma nzima ya uinjilishaji. Katekisimu ambayo ni muhtasari wa Imani ya Kanisa katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, Kanisa na Mambo ya nyakati. Ni muhtasari wa adhimisho la Fumbo la Pasaka katika Sakramenti za Kanisa, Sakramenti za Kristo, Sakramenti za wokovu, imani na uzima wa milele. Lengo ni kumtukuza Mwenyezi Mungu na mwanadamu kutakatifuzwa. Katekisimu ni muhtasari wa dira na mwongozo wa maisha ya kikristo unaofumbatwa katika Amri kumi za Mungu zinazopaswa kumwilishwa katika uhalisia wa maisha: kwa kuonesha upendo kwa Mungu na jirani, kama muhtasari wa Mafundisho makuu ya Kristo Yesu. Katekisimu ni muhtasari wa Maisha ya Sala kama ilivyokuwa kwenye Agano la Kale na Sala kuu ya Baba Yetu kama ilivyofundishwa na Kristo Yesu kwa kubeba muhtasari wa mafundisho mazito katika maisha na utume wake. Hii ni kazi iliyovaliwa njuga na Mtakatifu Yohane Paulo II kama chombo muhimu sana cha maisha na utume wa Kanisa katika kukabiliana na changamoto mamboleo. Hiki ni chombo cha majadiliano ya kiekumene, ili umoja katika imani ambayo ni chemchemi na msingi wake ni Fumbo la Utatu Mtakatifu, ienezwe hadi miisho ya dunia. Katekisimu ya Kanisa Katoliki inafumbata utajiri mkubwa wa: Maandiko Matakatifu, Mababa wa Kanisa, Mafundisho ya Mitaguso Mikuu, Mchango na mafundisho ya waalimu wa Kanisa, Watakatifu na viongozi wa Kanisa. Katekisimu iliidhinishwa rasmi kwa Waraka wa Mtakatifu Yohane wa Pili “Fidei depositum” yaani “Amana ya Imani” uliosindikiza kuchapishwa kwa Katekisimu ya Kanisa Katoliki, hapo tarehe 11 Oktoba 1992 na kuanza kutumika rasmi kama kitabu cha kufundishia: Imani, Sakramenti za Kanisa, Maadili na Maisha ya Sala ya Kanisa Katoliki tarehe 15 Agosti 1997.

Uteuzi Libya
19 May 2023, 15:03