Kard.Parolin:Makubaliano nchini Ukraine yanawezekana&ni dharura
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Wokovu wa sayari hatimaye ni suala la mkakati. Kuna mikakati ya ushiriki, ya mazungumzo ya kweli, ya ishara ya uaminifu, yenye uwezo wa kushinda ugumu wa chuki na majeraha ambayo kila mzozo husababisha kila mahali. Na kuna njama za vita kinyume chake ambazo huchochea masilahi ya washiriki, vurugu, unyanyasaji, ukoloni wa kiuchumi na kiitikadi, sheria ya wenye nguvu zaidi. Haya yanatoka katika mahojiano yaliyomo kwenye gazeti la kila juma la Kiitaliano liitwalo “Famiglia cristiana,” ya Katibu wa Vatican, Kardinali Pietro Parolin ambapo katika mahojiano hayo amebainisha kwamba "hakuna shaka kwamba kwa aina ya pili ya mpango, ubinadamu unahatarishwa kuanguka katika hali ya kutorudi tena na yenye matokeo mabaya.
Haiwezekani kuwaepo haki bila msamaha
Katibu wa Vaticani katika mahojiano yaliyo chapichwa katika toleo, Alhamisi tarehe 13 Oktoba 2022, yamechochewa na wito wa Papa Francisko ambao amekuwa akitoa mara kwa mara tangu mwezi Februari mwaka huu na kuendelea akipendelea kumalizika kwa janga la vita ambalo limeikumba nchi ya Ukraine na kulea maafa makubwa. Kwa upande wake Kardinali Parolin katika ndondoo hizi amebainisha anavyoona mapatano hayo kuwa sio tu yanawezekana, lakini pia ni ya lazima na ya dharura. Hata hivyo amesisitiza kuwa amani inajengwa juu ya haki na usawa. Akinukuu maneno ya Mtakatifu Yohane Paulo wa II, alisema: “hakuna haki bila msamaha.” kwa maana hiyo kusamehe, kwa upande wake, kunahitaji kugeuzwa, kuwa na "badiliko la mtazamo linalooneshwa katika matendo.”
Ni muhimu kukomesha mapigano ya silaha
Kardinali Parolin kwa njia hiyo hatabiri chochote kwa sababu amesema yeye hayuko katika nafasi ya kusema amani inawezekana, japokuwa na uhakika kuwa kukomesha mgogoro wa silaha, ulipuaji wa mabomu, uharibifu, ni hatua ya kwanza ya lazima. Ni hatua, ambayo lazima iambatane na kupendelewa na sio kwa ishara za vitisho, lakini kwa ishara za uaminifu na nia njema, ambayo hutengeneza mazingira ya mazungumzo na kufungua njia ya mazungumzo. Na kwamba Papa Francisko amekuwa wazi kuhusiana na suala hilo.
Licha ya hayo yote umuhimu wa kufungua mazungumzo
Kwa bahati mbaya, Kadinali Parolin amesema, "tumekuwa karibu kuzoea habari kuhusu vita na sio tu kwamba tunaona mapatano hayo yanawezekana," hivyo ana matumaini ya wito wa Papa Francisko kuwa unaweza kusikilizwa. Na ni kwa roho hiyo kwamba, anaamini, licha ya kutokuelewana, milango inabaki kuwa wazi na mazungumzo hayakatizwi kuhusiana na mkutano unaowezekana siku moja kati ya Papa na Kirill, Patriaki wa Korthodox wa Urussi wa Moscow. Kardinali amasema kwa upande wa Vatican, hamu haijawahi kupungua, hata kama hali imeizuia kuwa kweli. Hivyo wanahisi kwamba kuna shauku hiyo pia kwa upande wa Kanisa Kiorthodox.
Tusisahau vita vingine vilivyo wazi ulimwenguni
Wakati huo huo, Katibu wa Vatican Kardinali Parolin katika mahojiano hayo amebainisha kuwa sio hali ya Ukraine pekee yake inayomhusu Papa kwa sababu hatupaswi kusahau mikasa mingine kama ile ya Siria, Yemen na Tigray, na kuongezeka kwa mivutano katika Mashariki ya Kati na kwingineko. "Hata kama migogoro mingine haijatangazwa sana, hakuna vita ambavyo vina huzuni zaidi kuliko vingine; hakuna maisha yenye thamani ndogo kuliko nyingine", alisisitiza Kardinali Parolin.