Papa,Welby na Mwalace wametuma ujumbe wa Pasaka kwa viongozi wa kisiasa Sudan Kusini
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Katika ujumbe wa Pasaka kwa viongozi wa kisiasa wa Sudan Kusini, ambao umetiwa saini na Baba Mtakatifu Francisko, Askofu Mkuu Justin Welby wa Canterbury, Uingereza, na Mkuu wa Kanisa la Scotlanda, Mchungaji Jim Mwallace wanamebainisha kwamba “katika wakati huu wa kipindi cha Pasaka, tunawaandikia ili kushirikishana nanyi furaha yetu wakati tunasheherekea ufufuko wa Yesu Kristo, ambaye anatuonesha kuwa njia mpya inawezekana: njia moja ya msamaha na ya uhuru ambayo inaruhusu kuona kwa unyenyekevu Mungu kwa wengine, hadi kwa maadui zetu".
Uzoefu wa tumaini la Pasaka uwe chachu
Ujumbe huo unaendelea kueleza kwamba "Mchakato wa safari hiyo unafikisha katika maisha mapya, yawe kwa ajili yetu kama watu na iwe kwa ajili ya wale ambao tunawaongoza. Ni sala yetu ambayo mnaweza kuikumbatia kwa upya njia hiyo na hatimaye kuweza kufanya mang’amzi mapya ya njia katikati ya changamoto na mapambano ya wakati huu. Tunasali hata kwa ajili ya watu wenu waweze kufanya uzoefu wa matumaini ya Pasaka kwa njia ya uongozi wenu. Katika matarajio ya Hija yetu ya amani wakati wa kiangazi, tunasubiri kwa hamu kutembelea nchi yenu kubwa”. Inahitimishwa barua hiyo.
Ziara ya kitime barani Afrika DRC na Sudan Kusini
Ilikuwa ni mnamo tarehe 3 Mach 2022, wakati Ofisi ya Vyombo vya Habari vya Vatican ilithibitisha juu ya safari ya Papa kwenda nchini Sudan Kusini, nchi ambayo ataitembelea mara baada ya kuitembelea nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC mnamo tarehe 2 hadi 5, Julai 2022. Wakati ziara ya kitume y anchini Sudan Kusini imepangwa kuanzia tarehe 5 hadi 7 Julai, ambapo atatua jiji la Juba. Taifa hili changa daima limekuwa katika moyo wa Papa Fransisko, lililozaliwa na vita vya umwagaji damu na Sudan ambavyo vilimalizika kwa tangazo la uhuru mnamo 2011. Ukurasa mpya ulioangaziwa na matokeo chungu ya mzozo huo na hali ya kushangaza ya kibinadamu.
2019 viongozi wa Sudan Kusini walifanya mafungo Vatican
Kwa sababu hiyo, Papa Francisko mnamo mwezi Aprili 2019 alikuwa amewaita mamlaka ya juu zaidi ya kidini na kisiasa ya Sudan Kusini pamoja na Askofu Mkuu wa Canterbury Justin Welby kwenye Nyumba ya Mtakatifu Marta kwa ajili ya mafungo ya kiroho ya kiekumene. Katika nchi hiyo dhehebu kubwa la kidini ni Waanglikani. Kwa hakika mpango huo ulimalizika kwa ishara muhimu ya Papa ambaye alibusu miguu ya viongozi wa Sudan Kusini kwa ajili ya kuomba amani. Na wazo la safari ya kwenda Sudan Kusini lilikuwa tayari imefikiriwa tangu mnamo 2017, wakati Papa Francisko alipokutana na jumuiya ya kianglikana ya Roma katika Kanisa la Watakatifu Wote.