Baba Mtakatifu amekutana na Waziri wa Japan:kusitishwa wa silaha ni wazo kuu
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Jumatano tarehe 4 Mei 2022, kabla ya Katekesi yake, Baba Mtakatifu Francisko amekutana na kuzungumza karibu dk. 25 na Waziri Mkuu wa Japan Bwana Fumio Kishida, ambaye mara baada ya mazungumzo hayo amekutana pia na Kardinali Pietro Parolin, Katibu wa Vatican akiambatana na Askofu Mkuu Paul Richard Gallagher, Katibu wa Vatican kwa ajili ya Mahusiano na ushirikiano na Nchi. Kwa mujibu wa msemaji wa vyombo vya habari Vatican Dk. Mateo Bruni, kwa wandishi wa Habari amesema kuwa wakati wa mazungumzo yao na katibu wa Vatican, wameonesha kupendezwa kwa ushirikiano uliopo kwa pande mbili na kukumbusha miaka 80 tangu kuanza mahusiano yao ya kidiplomasia.
Katika muktadha huo aidha wamesisitiza na kupongeza mchango wa Kanisa Katoliki katika sekta mbali mbali za jamii ya Japan. Wakiendelea na mazungumzo yao wamekabiliana pia na masuala yenye tabia ya kimataifa kwa kuwa na umakini hasa vita nchini Ukraine huku wakisisitiza dharura ya mazungumzo na amanina wakiwa wanatarajio vita hivi viweze kuisha na dunia iwe huru bila silaha za kinyuklia.
Kumbu kumbu ya Hiroshima
Hata hivyo sio kwa mara ya kwanza kwa Papa Francisko anagusia maoni kuhusu upinzani wa muda mrefu kwa silaha za nyuklia. Wakati wa kumbukumbu ya miaka 75 ya shambulio la nyuklia huko Hiroshima, alituma ujumbe kwa waandaaji wa ukumbusho wa kumbukumbu hiyo, huku akikumbuka kwamba alisali kwenye kumbukumbu ya amani ya Hiroshima wakati wa ziara yake ya 2019 nchini Japan na alikutana na walionusurika. “Haijapata kuwa wazi zaidi kwamba, ili amani iweze kustawi, watu wote wanahitaji kuweka chini silaha za vita, na hasa silaha zenye nguvu zaidi na haribifu: silaha za nyuklia ambazo zinaweza kulemaza na kuharibu miji yote, nchi nzima”.
Wakati wa ziara yake ya 2019 nchini Japan, Papa Francisko alielezea umiliki au usambazaji wa silaha za atomiki kuwa mbaya. Pia yeye mara kwa mara ametoa wito wa kukomeshwa na kueleza kuunga mkono Mkataba wa Kuzuia Silaha za Nyuklia.