Papa atafunga Juma la Kuombea Umoja wa Wakristo
Na Sr. Angela Rwezaula, - Vatican.
Katika taarifa kutoka Ofisi ya Mshahereheshaji inasema kuwa Jumanne tarehe 25 Januari 2022, mida ya saa 11:30 jioni, majira ya Ulaya katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo Nje ya Ukuta, Baba Mtakatifu anatarajia kuadhimisha Masifu ya Pili ya Jioni, katika Siku Kuu ya Uongofu wa Mtakatifu Paulo Mtume, sambamba na Kuhitimisha Juma la Kuombea Umoja wa Wakristo ambapo mwaka huu linaongozwa na kauli mbiu kutoka kifungu cha Injili ya Matayo kisemacho: “Tuliona Nyota huko Mashariki na tumekuja hapa kumwambudu”(Mt 2, 2). Mwaka jana Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo alikuwa ameongoza maadhimisho hayo kwa niaba ya Baba Mtakatifu kutokana na kwamba alikuwa anaumwa.
Kwa maana hiyo tukio la kiutamaduni la Juma la Kuombea Umoja wa Wakristo kwa mwaka 2022 litaanza tarehe 18 hadi 25 Januari na ambalo litahusisha Makanisa na madhehebu yote ya Kikristo ulimwenguni kote. Mada ya mwaka 2022 imechaguliwa na Baraza la Makanisa ya Mashariki kwa kutaka kutafakari juu ya uzoefu wa Mamajusi. Katika mchakato wa Juma zima, Jumuiya zote zinaalikwa kutafakari juu ya mantiki maalum hasa kwa mada hiyo.
Kuanzia siku ya kwanza itaongozwa na kifungu muhimu cha tafakari: “Tuliona nyota ikichomoza”, ndiyo itakuwa tafakari ya siku ya kwanza na wakati siku ya pili itaongozwa na mada: “Mtoto huyo anapatikana wapo aliyezaliwa, Mfalme wa Wayahudi? Siku ya Tatu itakuwa: "Maneno hayo yaliwaletea wasi wasi mkubwa wakazi ya Yerusalemu na hasa Mfalme Herode". Siku ya Nne itajikita na mada: “Na wewe, Betlehemu, sio mji mdogo kabisa”. Siku ya Tano sentensi itakayoongoza tafakari ni: “Tazama, ile nyota waliyoiona mashariki ikawatangulia”. Katika siku ya sita ya tafakari itakuwa ni: “Wakamwona mtoto pamoja na Maria mamaye, wakaanguka kifudi fudi wakamsujudia”. Katika siku ya saba wanaalikwa kusali kwa ajili ya zawadi za Mamajusi: “wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na manemane. Na hatimaye pendekezo la siku ya nane na ya mwisho: “Nao wakaenda zao kwao kwa njia nyingine na kurudi kwao".