Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu mkuu Leo Boccardi kuwa Balozi wa Vatican nchini Japan. Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu mkuu Leo Boccardi kuwa Balozi wa Vatican nchini Japan. 

Askofu mkuu Leo Boccardi Balozi wa Vatican Nchini Japan

Askofu mkuu Leo Boccardi alizaliwa tarehe 15 Aprili 1953 huko San Martino in Pensilis, nchini Italia. Tarehe 24 Juni 1979 akapewa daraja Takatifu ya Upadre na Mtakatifu Yohane Paulo II. Mwaka 1987 akajiunga na Diplomasia ya Kanisa. Tarehe 18 Machi 2007 akawekwa wakfu kuwa Askofu mkuu. Amewahi kuwa Balozi wa Vatican: Sudan Kongwe, Eritrea, Iran na sasa anakwenda Japan.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko ameteua Askofu mkuu Leo Boccardi kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Japan. Kabla ya uteuzi huu, Askofu mkuu Leo Boccardi alikuwa ni Balozi wa Vatican nchini Iran. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Leo Boccardi alizaliwa tarehe 15 Aprili 1953 huko San Martino in Pensilis, nchini Italia. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, tarehe 24 Juni 1979 Mtakatifu Yohane Paulo II akampatia Daraja Takatifu ya Upadre. Tarehe 13 Juni 1987 akajiunga na Diplomasia ya Kanisa na kubahatika kuhudumia katika balozi kadhaa za Vatican.

Ilikuwa ni tarehe 16 Januari 2007, Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI alipomteuwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Sudan Kongwe na Eritrea na hivyo kumpandisha hadhi kuwa Askofu mkuu. Tarehe 18 Machi 2007 akawekwa wakfu kuwa Askofu mkuu na Kardinali Tarcisio Pietro Evasio Bertone, S.D.B. Aliyekuwa Katibu mkuu wa Vatican wakati huo. Ibada hii iliadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Padre Pio wa Pietrelcina, huko San Giovanni Rotondo, Italia. Tarehe 11 Julai 2013, Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Iran. Na ilipogota tarehe 11 Machi 2021 akamteuwa tena Askofu mkuu Leo Boccardi kuwa Balozi wa Vatican nchini Japan ili kuziba pengo lililoachwa wazi na Askofu mkuu Joseph Chennoth aliyezaliwa kunako tarehe 13 Oktoba 1943 na kufariki dunia tarehe 8 Septemba 2020.

Uteuzi Japan
14 March 2021, 14:19