Askofu mkuu Charles John Brown ameteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Ufilippini Askofu mkuu Charles John Brown ameteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Ufilippini 

Askofu mkuu Charles J. Brown: Balozi Wa Vatican Nchini Ufilippini

Askofu mkuu Charles John Brown alizaliwa mwaka 1959, huko New York, Marekani. Tarehe 13 Mei 1989 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. Kunako mwaka 1994 akaanza utume wake katika diplomasia ya Kanisa. Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI, tarehe 26 Novemba 2011, akamteua kuwa Askofu mkuu na Balozi wa Vatican nchini Ireland na kuwekwa wakfu tarehe 6 Januari 2012.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu mkuu Charles John Brown kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Ufilippini, kabla ya uteuzi huu Askofu mkuu Brown alikuwa ni Balozi wa Vatican nchini Albania. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Charles John Brown alizaliwa tarehe 13 Oktoba 1959, huko New York, Marekani. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, kunako tarehe 13 Mei 1989 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. Kunako mwaka 1994 akaanza utume wake katika diplomasia ya Kanisa.

Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI kunako tarehe 26 Novemba 2011, akamteua kuwa Askofu mkuu na Balozi wa Vatican nchini Ireland na kuwekwa wakfu tarehe 6 Januari 2012 na Kardinali Tarcisio Pietro Evasio Bertone, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Katika maisha na utume wake, amewahi kuwa Katibu mwambata wa Tume ya Taalimungu Kimataifa kuanzia mwaka 2009 hadi mwaka 2011. Balozi wa Vatican nchini Ireland tangu mwaka 2011 hadi mwaka 2017. Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Algania kuanzia mwaka 2017 hadi mwaka 2020. Tarehe 28 Septemba 2020 Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Ufilippini.

29 September 2020, 14:41