Kard.Ayuso Guixot:Wito wa mshikamano na udugu kwa ndugu Waislamu!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Kardinali Miguel Ángel Ayuso Guixot Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini, akihonjiwa na mwandishi wa Vatican News kuhusiana na Sikukuu ijayo ya Mwisho wa mwezi wa Ramadhani kwa ndugu zetu waislam, ambao hivi karibuni wameanza mfungo wa mwezi Mtukufu, amesema ni siku kuu yenye maana kuu kwa marafiki zetu waislamu.
Wakristo na waislamu waonyeshe mshikano wa ubinadamu
Kardinali amesema kwamba “ kama ilivyo kuwa kwetu sisi, kwa kipindi cha Pasaka, hata kwao mwaka huu, inaleta maana kubwa kwa namna ya pekee ndani ya janga la virusi vya corona au covi-19”. Kwa mujibu wa Kardinali anafikiri kuwa Ramadhani imechukua mwelekeo wa kiundani zaidi kwa mwaka huu kwa sababu katika hali ya kijumuiya haitawezekana kusherehekewa. Hii ndiyo sababu anapendelea kama Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini (PCDI) kuzidisha heri na matashi mema kwamba, Wakristo na Waislamu walioungana katika roho ya udugu, wanaonyeshe mshikamano na ubinadamu uliokumbwa na ugumu na watoe maombi yao kwa Mungu mwenyezi na wa huruma ili aweze kuleta ulinzi na kinga Yake juu ya kila kiumbe ili wakati huu mgumu uweze kumalizika.
Mada ya Hati ya Udugu wa kibinadamu
Kardinali Guixot aidha akitoa mantiki iliyomo katika ujumbe kwa mwaka huu amesema kuwa, Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini kila mwaka wanapendekeza mada ya pamoja kwa Jumuiya ya Kiislam na kwa pande zote mbili za dini. Kwa namna ya pekee, mwaka huu amesema, tumesisitiza mada kuhusu “ulinzi mahali pa ibada”, unaoongozwa na Hati ya Udugu wa Kibinadamu, ambapo Papa Francisko, pamoja na Imam Mkuu wa Al Azhar, walisema kwamba “ulinzi wa maeneo ya ibada ni jukumu la kuhakikishia na dini, maadili ya mwanadamu, sheria na mikataba ya kimataifa. Shambulio lolote au tishio ni kupotosha kwa mafundisho ya dini, na vile vile ukiukwaji wa dhahiri ya sheria za kimataifa, ambazo zinahukumiwa na waumini na wasio waumini. Hitaji la uhuru wa kuabudu na kufanya ibada ni haki na jukumu”.
Kwa njia ya mshikamano na udugu tunaweza kuwa bora zaidi ya zamani
Kardinali Ayuso Guixot, akijibu swali juu ya uhusiano gani wa mazungumzo uliopo kati ya watu wa dini tofauti na hali halisi katika mantiki ya wakati endelevu, amethibitisha kuhisi jukumu la kurejea kwa kile ambacho Papa Francisko katika ukweli huu mgumu amezidi kualika kueneza kwa namna ya pekee ‘usambazi wa tumaini’ ili kukabiliana na changamoto za sasa na zile za siku za usoni ambazo zitaona viongozi tofauti wa kidini wanaoalikwa kukuza umoja, mshikamano na udugu, kwa sababu anaongeza kusema kuwa, katika wakati huu wote tunaweza kweli kuwa bora zaidi kuliko tulivyokuwa zamani na kusaidia jamii zetu kuwa tayari kubadilisha kila kitu ambacho ni muhimu, bila kufuata sheria tu za uchumi na za faida.