Mshikamano na familia ya Mungu nchini Italia! Yataka moyo!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Familia ya Mungu nchini Italia, Jumanne tarehe 31 Machi 2020 ilisimama kwa muda wa dakika moja, kwa ajili ya kusali na kuwaombea wananchi wote waliofariki dunia kwa siku za hivi karibuni kutokana na homa ya mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona, COVID-19. Dr. Matteo Bruni Msemaji mkuu wa Vatican katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, amesema kwamba, Vatican pia imeungana na Serikali ya Italia kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea wale wote waliofariki dunia kutokana na ugonjwa wa Corona kwa kupandisha bendera nusu mlingoti. Hii ni ishara ya mshikamano wa huruma na upendo kwa watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaopambana kufa na kupona dhidi ya ugonjwa wa mapafu unaosababishwa na Virusi vya Corona, COVID-19.
Takwimu zilizotolewa na Serikali ya Italia zinaonesha kwamba, hadi kufikia tarehe 1Aprili 2020 Majira ya Saa 12: 00, Idadi ya watu waliokuwa wameambukizwa na Virusi vya Corona, COVID-19 walikuwa ni 80, 572. Wagonjwa waliofariki dunia hadi kufikia wakati huu ni 13, 155. Jitihada za madaktari na wauguzi zzimefanikiwa kuokoa maisha ya watu 16, 847. Katika hali tete namna hii, bado kuna haja ya kuzingatia itifaki ya mapambano dhidi ya ugonjwa wa homa ya mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona, COVID-19. Hakuna sababu msingi za kutaharuki, lakini watu wanapaswa kuwajibika kulinda na kudumisha Injili ya uhai dhidi ya kifo kwa kufuata masharti yaliyowekwa!