Tafuta

Mheshimiwa Padre Augusto Zampini ameteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Katibu Mwambata, Baraza la Kipapa la Maendeleo Fungamani ya Binadamu! Mheshimiwa Padre Augusto Zampini ameteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Katibu Mwambata, Baraza la Kipapa la Maendeleo Fungamani ya Binadamu! 

Padre Augusto Zampini, Katibu Mwambata: Maendeleo Fungamani!

Padre Zampini alizaliwa tarehe 25 Julai 1969 huko Buenos Aires, nchini Argentina. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, tarehe 22 Oktoba 2004 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre na kuingizwa Jimboni Isidro, nchini Argentina. Kabla ya kujiunga na malezi na makuzi ya wito wa Kipadre, aliwahi kufanya kazi kama wakili katika taasisi mbali mbali za kifedha nchini Argentina.

Na Padre Richard A. Mjigwa, - Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa Padre Augusto Zampini kuwa Katibu Mwambata wa Baraza la Kipapa la Huduma ya Maendeleo Fungamani ya binadamu. Kabla ya uteuzi huu, Padre Augusto Zampini, mwenye umri wa miaka 50 alikuwa ni afisa mwandamizi katika Baraza hili. Padre Zampini alizaliwa tarehe 25 Julai 1969 huko Buenos Aires, nchini Argentina. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, tarehe 22 Oktoba 2004 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre na kuingizwa Jimboni Isidro, nchini Argentina. Kabla ya kujiunga na malezi na makuzi ya wito wa Kipadre, aliwahi kufanya kazi kama wakili katika taasisi mbali mbali za kifedha nchini Argentina. Ni Padre aliyefanikiwa kujiendeleza zaidi katika masomo ya taalimungu na taalimungu maadili na baadaye alijipatia pia shahada ya uzamivu kuhusiana na masuala ya tafiti za kisayansi kutoka Chuo Kikuu cha Cambrigde, Uingereza.

Lakini, kimsingi, Padre Augusto Zampini ni mtaalamu aliyebobea katika masuala taalimungu maadili na zaidi sana katika mambo ya kiuchumi na kanuni maadili kuhusu mazingira. Kutokana na uelewa wake mpana, alibahatika kwa miaka kadhaa kufundisha vyuo vikuu kadhaa nchini Argentina na Uingereza. Tangu mwaka 2017 alipewa dhamana ya kuratibu masuala ya “Imani na Maendeleo” eneo linalofumbata kwa namna ya pekee masuala ya uchumi na fedha; makundi ya kijamii, ajira, idadi ya watu, amani na maendeleo mapya ya sayansi na teknolojia! Huduma yote hii amekuwa akiitekeleza kwenye Baraza la Kipapa la Huduma ya Maendeleo Fungamani ya binadamu. Kunako mwaka 2018, Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa kuwa ni kati ya wataalam walioshiriki katika maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu Ukanda wa Amazonia, mwezi Oktoba, 2019. Pamoja na shughuli zote hizi, pia ni mwanachama wa vyama vya kitaalimungu nchini Argentina na Barani Ulaya katika ujumla wake.

Katibu Mwambata

 

 

10 April 2020, 14:56