Askofu Zolite Peter Mpambani ateuliwa kuwa Askofu mkuu wa Bloemfontein!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko ameridhia ombi la kutaka kung’atuka kutoka madarakani lililowasilishwa kwake na Askofu mkuu Jabulani Adatus Nxumalo, O.M.I wa Jimbo kuu la Bloemfontein, Afrika ya Kusini. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteua Askofu Zolile Peter Mpambani, S.C.I., kutoka Jimbo Katoliki la Kokstad, Afrika ya Kusini kuwa Askofu mkuu mpya wa Jimbo Kuu la Bloemfontein. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu mteule Zolile Peter Mpambani alizaliwa tarehe 20 Februari 1957 huko Umlamli, Jimbo Katoliki la Aliwal. Tarehe 28 Januari 1982 akaweka nadhiri zake za daima. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, tarehe 25 Aprili 1987 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre.
Tangu wakati huo, amewahi kuwa ni Paroko usu, Paroko na Mlezi wa Wanovisi; Mshauri wa Shirika kwa ajili ya Afrika na Madagascar, kwenye Makao Makuu ya Shirika yaliyoko mjini Roma. Kati ya Mwaka 2005-2010 aliteuliwa kuwa Mlezi wa Wanovisi, Mkuu wa nyumba. Kati ya Mwaka 2011 hadi mwaka 2013 alikuwa ni Paroko wa Parokia Sterkspruit, Jimbo Katoliki la Aliwal. Kati ya Mwezi Februari hadi Mei 2013, alichaguliwa kuwa Mkuu wa Shirika Kanda ya Afrika ya Kusini. Tarehe 6 Mei 2013 akateuliwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Kokstad na hatimaye, kuwekwa wakfu hapo tarehe 3 Agosti 2013.