Mons. Luis Munoz Cardaba: Balozi mpya wa Vatican Sudan na Eritrea
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko amemteua Monsinyo Luís Miguel MUÑOZ CÁRDABA kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Sudan na Eritrea pamoja na kumpandisha hadhi kuwa Askofu mkuu. Askofu mkuu mteule Luís Miguel MUÑOZ CÁRDABA alizaliwa tarehe 25 Agosti 1965 huko Vallelado, nchini Hispania. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, tarehe 28 Juni 1992 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. Alijiendeleza na hatimaye kubahatika kupata Shahada ya Uzamili katika masomo ya taalimungu, Sheria za Kanisa pamoja na Sheria na Taratibu za Uendeshaji wa Kesi Mahakamani, “Giurisprudenza”.
Askofu mkuu mteule Luís Miguel MUÑOZ CÁRDABA alianza kutoa huduma za Kidiplomasia mjini Vatican hapo tarehe 1 Aprili 2001. Tangu wakati huo ametumwa kwenye Balozi za Vatican nchini Ugiriki, Mexico, Ubelgiji, Italia, Australia, Ufaransa na Uturuki.