Waziri Mkuu wa Montenegro akutana na Papa Francisko
Na Padre Richard A. Mjigwa, - Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 14 Desemba 2019 amekutana na kuzungumza na Bwana Duško Marković, Waziri mkuu wa Montenegro, ambaye baadaye, amekutana na kuzungumza pia na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, Katibu mkuu wa Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican. Baba Mtakatifu pamoja na mgeni wake, katika mazungumzo yao, wamegusia kuhusu uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizi mbili na kwamba, wameonesha utashi wa kutaka kuuimarisha zaidi.
Viongozi hawa kwa pamoja wamekazia umuhimu wa watu wa Mataifa kuishi kwa amani, umoja na mshikamano kwa kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini, kiekumene na kitamaduni; mambo msingi katika maisha na utambulisho wa wananchi wa Montenegro. Mwishoni mwa mazungumzo yao, wamejielekeza zaidi kwenye tema za kikanda na kimataifa, hususan hatima ya Umoja wa Ulaya na changamoto zake bila kusahau wimbi kubwa la wakimbizi na wahamiaji duniani!