Noeli isaidie kuaminiana na kushirikiana kwa ajili ya wema wa wote!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Kardinali Gualtiero Bassetti Rais wa Baraza la Maaskofu Italia na Askofu Mkuu wa jimbo Kuu katoliki la Perugia-Città della Pieve, wakati wa kutoa matashi mema ya Sikukuu ya Noeli kwa Baraza zima la jimbo lake kama vile wahusika na wahudumu wa ofisi na huduma za jimbo kuu, amewambia kuwa “Noeli ni fumbo la Bwana kujifanya mtu. Hii inakuwa fursa ya kujikita kwa upya katika zawadi ya matunda ya amani ndani ya mioyo yetu, mahali pa kazi, ndani ya familia na katika jumuiya zetu”.
Kuna haja ya mwanga katika mji
Akiendelea na hotuba yake Kardinali Bassetti ameweka mtazamo wake katika jamii na kusema: “Leo hii kuna haja ya kuwa na mwanga kwa ajili ya mji wetu, nchi yetu na zaidi kuna haja ya kuwa wawazi kwa upande wetu wote, hasa kuanzia na wale wote ambao wanawajibika katika Kanisa na katika serikali na Taasisi za Umma. Tunapaswa daima kuaminiana sisi kwa sisi na wengine; tunapaswa kushirikiana kwa ajili ya wema wa wote”.
Urari wa kichungaji kwa mwaka 2019
Kardinali Bassetti pia ameweza kuonesha hata urari wa kichungaji kwa mwaka ambao huko ukingoni, huku akikugusa muktadha husika na maeneo ambayo ni muhimu kwenye maisha ya uinjilishaji na shughuli za kimisionari za Kanisa la Jimbo. Ya kwanza kabisa ni miito ya kikuhani na maisha ya kitawa ambayo amethibitisha kuwa “baada ya miaka kadhaa ya kuchanua, leo hii inazidi kupungua sana”.
Mantiki nyingine ya kichungaji ni ile ya hisani na huduma ya watu
Mantiki nyingine ya kichungaji ambayo imekuwa na umakini wa Kardinali Bassetti ilikuwa inahusu juu ya kufanya hisani ya kidugu na utoaji wa huduma kwa watu na familia ambao wako kwenye shida kubwa za kiuchumi hasa kutokana na kupoteza kazi, na ambapo amesema Caritas ya Jimbo na Caritas ya Parokia ziko mstari wa mbele kabisa kwa njia ya mtandao wao wa shughuli mbalimbali kama ishara na muundo wa mapokezi ambayo hutoa ukarimu wa kupokea watu zaidi ya 300 kwa mwaka!
Baba Mungu endelea kufufua miito kwa vijana ya kujitolea
Shughuli hizi ambazo kama alivyokumbusha Kardinali ni matunda ya jitihada za kujitolea bure bila kujibakiza kwa watu wengi ambao wamekuwa na ari ya maana ya mshikamano kuhusu jirani. Na kwa maana hiyo Baraka zake ni kwamba “ Mungu Baba aendelee kufufua zaidi miito ya vijana katika kujitolea” amehitimisha.