Tafuta

Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu Mstaafu Alfred Kipkoech Arap Rotich wa Jimbo la Kijeshi Kenya kuwa Askofu mpya wa Jimbo la Kericho. Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu Mstaafu Alfred Kipkoech Arap Rotich wa Jimbo la Kijeshi Kenya kuwa Askofu mpya wa Jimbo la Kericho. 

Askofu Mstaafu Alfred Rotich, ateuliwa kuwa Askofu wa Kericho!

Askofu Alfred Kipkoech Arap Rotich alizaliwa mwaka 1957. Mwaka 1983 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. Tarehe 9 Machi 1996 akateuliwa kuwa Askofu Msaidizi wa Jimbo kuu la Nairobi na kuwekwa wakfu kuwa Askofu hapo tarehe 3 Julai 1996. Tarehe 29 Agosti 1997 akateuliwa kuwa Askofu wa Jimbo la Kijeshi nchini Kenya na kung’atuka kutoka madarakani tarehe 30 Desemba 2016.

Na Padre Richard A. Mjigwa, - Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko ameridhia ombi la kung’atuka kutoka madarakani lililowasilishwa kwake na Askofu Emmanuel Okombo Wandera wa Jimbo Katoliki la Kericho, nchini Kenya. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteua Askofu mstaafu Alfred Kipkoech Arap Rotich mwenye umri wa miaka 62 kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Kericho nchini Kenya. Askofu Alfred Kipkoech Arap Rotich alizaliwa tarehe 27 Julai 1957 huko Longisa. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, tarehe 18 Novemba 1983 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. Tarehe 9 Machi 1996 akateuliwa kuwa Askofu Msaidizi wa Jimbo kuu la Nairobi na kuwekwa wakfu kuwa Askofu hapo tarehe 3 Julai 1996. Tarehe 29 Agosti 1997, Mtakatifu Yohane Paulo II akamteuwa kuwa Askofu wa Pili wa Jimbo la Kijeshi nchini Kenya na kung’atuka kutoka madarakani tarehe 30 Desemba 2016. Baba Mtakatifu Francisko amemwangalia tena kwa kijicho la upendo wa kibaba, tarehe 14 Desemba 2019 akamteuwa kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Kericho! Matendo makuu ya Mungu!

Itakumbukwa kwamba, Jimbo la Kijeshi nchini Kenya lilianzishwa kunako tarehe 20 Januari 1964 na Hayati Kardinali Maurice Michael Otunga ambaye kwa sasa kuna mchakato wa kumtangaza kuwa Mwenyeheri unaendelea nchini Kenya, ndiye aliyekuwa Askofu wake wa kwanza. Mtumishi wa Mungu Otunga akaliongoza Jimbo hilikuanzia tarehe 20 Januari 1964 hadi tarehe 29 Agosti 1997. Mtakatifu Yohane Paulo II akamteuwa Askofu Afred Kipkoech Arap Rotich kuliongoza Jimbo hili la Kijeshi kuanzia tarehe 29 Agosti 1997 hadi tarehe 30 Desemba 2016 alipong’atuka kutoka madarakani. Jimbo liliundwa ili kusogeza huduma kwa familia ya Mungu katika vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na familia zao.

Askofu Kenya
14 December 2019, 11:57