Kard.Turkson:hata watumiaji wa samaki wawajibike katika jamii!
Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wavuvi ulimwenguni ambayo uadhimishwa kila ifikapo tarehe 21 Novemba ya kila mwaka Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Huduma na Maendeleo fungamani ya binadamu, ametoa ujumbe wake akitaka kufafanua wazi nini maana ya siku hiyo hasa ya kutoa kipaubele cha kusikiliza sauti za wavuvi na familia zao. Kardinali Turkson anashauri kwa namna ya pekee kukabiliana na mada iliyochaguliwa kuongoza kwa mwaka huu 2019 isemayo “Jukumu la kijamii katika mnyororo wa usambazaji wa samaki” na huku akiunganisha pamoja Wosia wa Laudato Si wa Baba Mtakatifu Francisko ambaye katika Wosia huo anasisitizia juu ya ulazima wa ekolojia fungamani. Katika ujumbe huo anatoa mwaliko hasawa kuzingatia jukumu la kijamii kwenye makampuni ya kimataifa na yale madogo madogo ya kifamilia kwa kushirikiana kati ya serikali mbali mbali na mamlaka za baharini ili kuangalia usalama wa haki za binadamu.
Majukumu ya watumiaji ambao watambue kununua ni tenda la kimaadili
Katika ujumbe wake kwa kukumbusha Waraka wa kitume wa Caritas in veritate juu ya maendeleo kamili ya mwanadamu katika upendo na ukweli, wa Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI, na ambao unazingatia muktadha wa sasa wa juhudi za kukuza maendeleo na kwa ajili utimilifu wa kila binadamu, Kardinali Turkson amesema, lazima watumiaji wawajibike na ambao kwa uzito wa uchaguzi wao wanaweza kushawishi maamuzi na uchaguzi wa soko la makampuni. Ni vema watu wakatambua kuwa kununua ni tendo la kimaadili daima, zaidi ya kuwa uchumi. Kwa njia hiyo kuna ulazima wa uwajibikaji wa dhati kijamii kwa watumiaji ambao wanasindikiza ule uwajibikaji wa makampuni kijamii (Waraka wa Caritas in veritate wa Benedikto XVI,)”. Kwa njia hiyo ni dharura kwamba serikali hata kwa njia ya ushirikiano na mashirika ya kimataifa, kikanda na ya kijamii kukabiliana na masuala ya uwajibikaji kijamii katika sekta ya uvuvi na zaidi kwa ujumla wa sekta zote ambazo zinahusika na usafiri kati ya bahari na ubinadamu. Katika dunia jitihada za moja kwa moja katika sekta ya uvuvi na katika maisha ni karibia milioni 60 ya watu na miongoni mwao ni asilimia 14 ni wanawake wanajikita katika sekta hihii ya uvuvi.
Siku ya uvuvi ilianzishwa kunako 1997 na wavuvi wa New Delhi, India
Siku ya Uvuvi ulimwenguni ilianzishwa na Jumuiya ya wavuvi huko New Delhi- India kunako tarehe 21 Novemba 1997 . Ni kwa njia ya wawakilishi wa wavuvi na utamaduni,pamoja na wafanyakazi wa sekta ya baharini kutoka nchi 32 duniani ambapo waliungana pamoja kama njia mojawapo ya kusheherekea kazi hiyo inayowapatia kipato watu wengi duniani; vile vile na kuunda Shirika la Kimataifa kwa kujiwekea malengo ya kusaidiana katika matendo ya dhati ya uvuvi wa kudumu kwa ngazi ya ulimwengu na haki ya kijamii.
Changamoto za sekta ya uvuvi ni kupambana na uvuvi haramu
Hata hivyo katika kilele cha kuadhimisha siku ya kimataifa ya kupambana na uvuvi haramu na usiofuata kanuni (IUU) kwa mwaka huu 2019 Shirika la chakula na kilimo (FAO) lilizitaka nchi zote duniani kuchukua hatua ya kufuata nyayo za Thailand ili kukabiliana na tatizo hilo linaloelekea kutanda mizizi yake. Shirika la FAO lilisema kuwa Thailand ambayo ni msafirishaji wa tatu mkubwa wa samaki duniani hivi sasa imeongeza juhudi za kupambana na uvuvi haramu ili kufikia lengo la rasilimali endelevu za baharí. Tangu mwaka 2015 Thailand ilitathimini upya sheria na mifumo yake na kisha kuandaa mpango wa kitaifa wa kuchukua hatua dhidi ya uvuvi haramu, usioripotiwa na usiofuata kanuni,( IUU). Miongoni mwa hatua hizo ni kufungua kituo cha ufuatiliaji wa masuala ya uvuvi katika idara ya uvuvi ya serikali ambacho kinahitaji vyombo vyote vya kimataifa vinavyovua kupatiwa leseni na kutumia mfumo maalum unaonasa shughuli zote za uvuvi au (VMS ) na pia kutekeleza programu ya ukaguzi kabla ya kuondoka na vinapowasili bandarini.
Uvuvi haramu na usiofuata kanuni ni kadiri ya tani milioni 26
Uvuvi haramu na usiofuata kanuni zinakadiriwa kuwa ni tani milioni 26 kwa mwaka au sawa na moja ya tano ya samaki wote wanaovuliwa kote duniani na mbali ya kupora rasilimali za jamii pia unachangia katika uharibifu wa mazingira ya bahari na kuathiri viumbe. Tarehe 5 Desemba 2017 Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliafiki kupitisha azimio lililopendekezwa na FAO kuhusu uvuvi endelevu na kuitangaza kunako tarehe 5 Juni ya kila mwaka kuwa ni siku ya kimataifa ya kupinga uvuvi haramu na usiofuata kanuni na maadhimisho ya kwanza yalifanyika mwaka mwaka 2018.