Askofu mkuu mteule Nicodème B. Bènissan, Jimbo kuu la Lomè, Togo
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko ameridhia ombi lililowasilishwa kwake na Askofu mkuu Denis Komivi Amuzu-Dzakpah wa Jimbo Kuu la Lomé nchini Togo la kutaka kung’atuka kutoka madarakani. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteua Askofu Nicodème Anani Barrigah-Bénissan kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Lomè, Togo, hadi kuteuliwa kwake, alikuwa ni Askofu wa Jimbo Katoliki Atakpamé. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu mteule Nicodème Anani Barrigah-Bénissan alizaliwa tarehe 19 Mei 1963 huko Ouagadougou nchini Burkina Faso.
Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, tarehe 8 Agosti 1987 akapewa daraja Takatifu ya Upadre. Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI kunako tarehe 9 Januari 2008 akamteuwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Atakpamè, lililoko nchini Togo na kuwekwa wakfu kuwa Askofu tarehe 9 Machi 2008. Na ilipofika tarehe 23 Novemba 2019, Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Lomè nchini Togo.