Baba Mtakatifu Francisko kwa barua yake binafsi "Sedula mater" ya mwaka 2016 alianzisha rasmi Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha. Baba Mtakatifu Francisko kwa barua yake binafsi "Sedula mater" ya mwaka 2016 alianzisha rasmi Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha. 

Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha: Miaka 3 ya kuanzishwa kwake!

Baba Mtakatifu Francisko kunako 15 Agosti 2016 katika barua yake binafsi, “Motu Proprio” “Sedula mater” alianzisha Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha kama sehemu ya mchakato wa Sekretarieti kuu ya Vatican kusoma alama za nyakati na kujibu kwa ufasaha na weledi mkubwa changamoto mamboleo katika maisha na utume wa Kanisa hususan katika maisha ya ndoa na familia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Injili ya Kristo ni chemchemi inayowapatia wanafamilia ari, nguvu na jeuri ya kutangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu kwa watu wa nyakati hizi kwa kuzingatia tunu msingi za Injili ya familia mintarafu Mafundisho ya Kanisa. Ili kuweza kukabiliana na changamoto zote hizi, Baba Mtakatifu Francisko kunako 15 Agosti 2016 katika barua yake binafsi, “Motu Proprio” “Sedula mater” alianzisha Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha kama sehemu ya mchakato wa Sekretarieti kuu ya Vatican kusoma alama za nyakati na kujibu kwa ufasaha na weledi mkubwa changamoto mamboleo katika maisha na utume wa Kanisa hususan katika maisha ya ndoa na familia.

Baba Mtakatifu katika barua hii anasema, Mama Kanisa, mwingi wa huruma na mapendo, katika historia ya maisha na utume wake, amekuwa karibu sana kwa waamini walei, familia pamoja na kuhimiza Injili ya uhai, kama kielelezo cha ufunuo wa huruma na upendo wa Kristo Yesu kwa walimwengu. Kanisa linatambua na kuthamini mchango wa waamini walei katika maisha na utume wake, kwani hawa wamepewa changamoto ya kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha, mwaka 2019 linaadhimisha kumbu kumbu ya Miaka mitatu tangu lilipoanzishwa. Tangu wakati huo, limeendelea kusimama kidete kulinda, kutetea na kudumisha Injili ya uhai dhidi ya utamaduni wa kifo.

Baraza linawahamasisha waamini walei kuhakikisha kwamba, wanalitegemeza Kanisa kwa karama na mapaji yao sanjari na kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini walei watambue: dhamana, wajibu na haki zao msingi ndani ya Kanisa. Vyama na mashirika ya kitume ni muhimu sana katika kufunda, kulea, kukuza na kudumisha imani inayomwilishwa katika matendo. Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican wanawahamasisha waamini walei kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Baraza liko mstari wa mbele katika kukuza na kudumisha utume wa vijana wa kizazi kipya, kwa kutambua kwamba, vijana ni jeuri na matumaini ya Kanisa kwa leo na kwa siku za usoni.

Wanawake

 

20 August 2019, 11:27