Zimechaguliwa mada tatu za kuongoza Siku ya vijana duniani kuanzia 2020-2022!
Na Sr Angela Rwezaula – Vatican
Taarifa kutoka Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha, wametangaza tarehe 22 Juni 2019 juu ya Mada ambazo zimechaguliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuongoza mchakato wa safari ya miaka mitatu ya maadalizi ya kuadhimisha Siku ya vijana duniani ambayo kilele cha maadhimisho hayo kimataifa itakuwa huko Lisbon Ureno mwaka 2022.
Mada ya siku ya vijana kwa mwaka 2020, 2021 na 2022
Siku ya XXXV ya vijana duniani mwaka 2020 itaongozwa na mada:“Kijana! Nakuamuru,amka!(Lk 7,14);Siku ya XXXVI Vijana duniani,2021 itaongozwa na mada, “Inuka! Nimekutokea uwathibitishie mambo uliyoona leo (Mdo 26,16);Siku ya XXXVII ya vijana duniani 2022 (Lisbon) itaongozwa na mada,“Maria alimka na kwenda kwa haraka”(Lk 1,39).
Safari ya kiroho iliyoelekezwa na Papa
Safari ya kiroho ambayo imeelekezwa na Baba Mtakatifu Francisko inakwenda sambamba na tafakari iliyoongozwa Siku ya vijana duniani mwaka 2019 na katika mchakato wa safari ya Sinodi kwa namna ya pekee kwa Wosia wa Kitume Christus vivit. Kwa njia yake katika (n. 20), Baba Mtakatifu anataja Injili ya Lk 7,14 kwa kuwashauri vijana waache il waguswa na nguvu ya Bwana mfufuka na kuanza kwa upya na nguvu ya kiundani katika ndoto, shauku, matumaini na ukarimu ambao ndiyo tabia ya maisha ya ujana wao.
Kinacho unganisha mada tatu ni mwaliko kwa vijana "kuamka”
Kile ambacho kinaunganisha mada hizo tatu kwa dhati ni mwaliko kwa vijana ili waamke kidete, kwa maana hiyo wanapaswa kukimbia ili waweze kuuishi wito wa Bwana na kutangaza Habari Njema kama alivyo fanya mama Maria, mara baada ya kupashwa habari alijibu, “ tazama mimi hapa”. Neno kuamka katika injili ya Luka ina maana ya kufufuka, au kuamka tena katika maisha mapya!
Kwa maelezo zaidi, unaweza kupata taarifa kutoka katika lugha ya kifaransa, kingereza, kireno na tafsiri rasimi ya mada hizo katikaTovuti ya Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha: http://www.laityfamilylife.va/content/laityfamilylife/it.html