Tafuta

Papa Francisko: Michezo inajenga na kudumisha tunu msingi za maisha ya kifamilia! Papa Francisko: Michezo inajenga na kudumisha tunu msingi za maisha ya kifamilia! 

Papa Francisko: Michezo inajenga na kudumisha tunu za kifamilia!

Jumapili, tarehe 26 Mei 2019 kumefanyika mashindano ya mpira wa miguu kati ya wanawake wanaofanya kazi mjini Vatican dhidi ya wanawake wa Jiji la Roma. Mchezo huu ulikuwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku kuu ya Familia, tukio ambalo liliziunganisha familia za wafanyakazi wa Vatican ili kusherehea zawadi ya maisha na utume wa familia. Michezo ni furaha, umoja na upendo!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Mama Kanisa anasema, michezo inayo nafasi muhimu sana katika mchakato wa uinjilishaji mpya, unaofumbatwa katika ushuhuda wenye mvuto na mashiko. Michezo ni nyenzo msingi katika kusimamia na kudumisha haki msingi za binadamu; ni njia inayomwelekeza mchezaji kwenye utakatifu. Michezo ni mahali muafaka pa kuonja uzuri na utakatifu wa kazi ya uumbaji, umoja, udugu na mshikamano wa kweli, unaovunjilia mbali ubinafsi kwa kukazia umoja katika ukweli wake!

Michezo ni muhimu sana katika ujenzi wa jamii na ushiriki mkamilifu katika kudumisha: haki, amani na utulivu bila vita, kinzani na mipasuko ya kijamii. Michezo inadumisha umoja na mshikamano wa familia. Jumapili, iliyopita, tarehe 26 Mei 2019 kumefanyika mashindano ya mpira wa miguu kati ya wanawake wanaofanya kazi mjini Vatican dhidi ya wanawake wa Jiji la Roma. Mchezo huu ulikuwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku kuu ya Familia, tukio ambalo liliziunganisha familia za wafanyakazi wa Vatican ili kusherehea zawadi ya maisha na utume wa familia

Ni katika muktadha huu, Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwenda kwa Monsinyo Domenico Ruggiero, Rais wa Idara ya Michezo Vatican, amewatakia heri na baraka washiriki wote wa kabumbu hilo lililosakatwa na wanawake. Imekuwa ni fursa ya kufahamiana, kushirikiana na kushikamana katika ujenzi wa umoja na udugu wa kibinadamu. Baba Mtakatifu anawataka wafanyakazi wa Vatican kuwa ni mfano bora wa kuigwa kama mashuhuda wa Kristo Mfufuka na Injili yake! Mwishoni, Baba Mtakatifu amewapatia baraka zake za kitume!

Parolin: Michezo
28 May 2019, 11:34