Janga la Moto Kanisa kuu la Notre Dame: Mwaliko kwa Papa Francisko
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, akiwa ameambatana na Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, Jumamosi, tarehe 20 Aprili 2019, amekutana na kuzungumza na Bwana Jean-Yves Le Drian, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Ufaransa. Dr. Alessandro Gisotti, Msemaji mkuu wa mpito mjini Vatican amethibitisha kwamba, mkutano huo uliofanyika mjini Vatican, umegusia kwa namna ya pekee kabisa ujenzi wa Kanisa kuu la Notre Dame, Jimbo kuu la Paris, Ufaransa lililoteketea kwa janga la moto hivi karibuni.
Bwana Jean-Yves Le Drian kwa niaba ya Rais Emmanuel Macron amemwalika Baba Mtakatifu Francisko kutembelea Ufaransa ili kujionea mwenyewe madhara makubwa yaliyosababishwa na janga la moto. Mwaliko huu umepokelewa kwa mikono miwili na kwamba, utaendelea kufanyiwa kazi na majibu kutolewa kwa wakati muafaka! Wakati huo huo, Rais Emmanuel Macron amesema, Serikali ya Ufaransa inatarajia kwamba, Kanisa kuu la Notre Dame, litaweza kufanyiwa ukarabati kwa muda wa miaka mitano na hivyo kurejea tena katika hali yake yenye mvuto na mguso kwa maisha ya kiroho, kitamaduni na kijamii. Ukarabati huu utazingatia msingi ya ukweli na uwazi katika kupokea na kutumia fedha zitakazochangwa na wadau mbali mbali.