Tarehe 2 Aprili 2005 Mtakatifu Yohane Paulo II aliaga dunia na mazishi kuudhuriwa na mamilioni ya watu toka pande zote za dunia Tarehe 2 Aprili 2005 Mtakatifu Yohane Paulo II aliaga dunia na mazishi kuudhuriwa na mamilioni ya watu toka pande zote za dunia 

Mt.Yohane Paulo II:Miaka 14 iliyopita Mtakatifu Yohane Paulo II aliaga dunia hii!

Ilikuwa ni tarehe 2 Aprili 2005,Mtakatifu Yohane Paulo II aliaga dunia hii.Umati wa watu kutoka pande zote za dunia walifika kutoa heshima na kushukuru utume wake aliotenda akiwa hapa duniani,waamini wa kila dhehebu,,familia,vijana,wanasiasa,wagonjwa na wazee,katika mwendelezo wa utume wa Mtakatifu Petro

Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican

Ilikuwa ni tarehe 2 Aprili 2005, saa 3.37 kifo kilimfikia, miaka 14 iliyopita Mtakatifu Yohane Paulo II.  Kwa masaa mengi sana, maelfu ya waamini walikuwa wamejaa uwanja wa Mtakatifu Petro wakisali Rosari Takatifu. Ni milioni 7 ya wanahija waliweza kufika mjini Roma katika siku zile za mateso kabla ya kifo chake na wakati wa mazishi, kwa aliyekuwa anajulikana kwa jina la ubatizo Karol Wojtyla!

Tangazo rasmi kuhusu kifo chake

Inakumbukwa siku ile uchungu ulitanda kwa watu wote, pamoja na shukrani lakini pia kuongozwa na imani ya kina kwa wale ambao, walijazwa furaha ya Papa kwa aliyekuwa amechaguliwa tarehe 16 Oktoba 1978. Aliye toa tangazo usiku wa mauti yake kwa waamini waliokuwa wameunganika chini ya  miguu ya Jengo la Kitume alikuwa ni katibu wa Msaidizi mjini Vatican, wa wakati huo Kardinali Leonardo Sandri. Katika siku zilizokuwa zinafuata, msululu mrefu usiosha wa watu kutoka duniani kote walifika mjini Vatican, kutoa heshima ya mwisho kwa mwili wa marehemu ambaye kabla ya miaka 10 ya kifo chake kunako tarehe 27 Aprili 2014 alitangazwa kuwa Mtakatifu.

Mazishi yake tarehe 8 Aprili 2005

Aliyeongozwa Misa ya mazishi, tarehe 8 Aprili 2005, alikuwa ni Kardinali Joseph Ratzinger, dekano wa Baraza la Makardinali, ambaye baada ya siku chache alichaguliwa mwenyewe kuwa Papa na kuchagua jina la Benedikto XVI. Tukiwa bado katika masikio na hisia zeti juu ya  Ziara ya Kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Morocco, ni wazi kuwa watu wengi watakuwa wameguswa pia na kugusia kwa mara nyingine hija za kichungaji zilizofanywa na Mtakatifu Yohane Paulo II, vile vile hata nchini Morocco. Hii ni kuonesha kwamba ni sehemu hai ya mchakato wa uinjilishaji na ushuhuda wa kimisionari.

Mchango mkubwa wa kitume wa Mtakatifu Yohane Paulo II

Mtakatifu Yohane Paulo II ametoa mchango mkubwa katika maisha kukuza na kudumisha utu, heshima, ustawi na maendeleo ya wanawake ndani na nje ya Kanisa. Itakumbukwa sana kwa ufunguzi wa  mkutano wa kidini na Majadiliano huko Assisi kunako tarehe 27 Oktoba  1986, hii ilikuwa ni ndoto kubwa na ambapo aliweweza kuwaalika viongozi wote dunia. Mkutano ulikuwa mzuri sana wa roho ya sala, na kadiri miaka  inavyopita mkutano huo unajulikana kwa jina la Roho ya Assisi. Alifanya hivyo kwa ajili ya kuinua mioyo ya watu kwa Mungu mmoja kwa lugha moja na wimbo wa amani. Wawakilishi kutokana nchi 70 wa madhehebu mbali mbali duniani waliweza kushirikishana matumaini katika dunia inayozidi kutamani ubora, ubunifu, udugu wa kina na ubinadamu wa dhati. Tukio hili lilikuwa linabeba ujumbe wake unaojikita katika tamaa ya amani, na unaoshirikishwa watu tu wenye mapenzi mema, kubaki wanatazama na kutenda kwa dhati, katika hali halisi ya dunia na kutafuta mahusiano kati ya watu tofauti. Amani inaweza kupatikana tu kwa njia ya mahusiano ya kina.

Mtakatifu Yohane Paulo II amekuwa kioo kwa vijana waliopita na wa kizazi kipya

Ni wazi kwamba moyo wa mapapa wote wa Kanisa wamekuwa na lengo kuu la kutafuta watu wa Mungu watambue umuhimu wa kutafuta amani. Ndilo jukumu la Kiongozi wa Kanisa sauti ya kanisa la Ulimwengi katika kuendeleza nyayo za waliopita zaidi ya miaka 2000. Aidha Mtakatifu Yohane Paulo II amekuwa kioo kwa vijana waliopita, wa kizazi kipya, waliompenda na wanao endelea kumpenda upeo, ambapo ni ushuhuda unao jionesha hadi wakati huu kwa njia ya maadhimisho ya Siku za Vijana kitaifa na kimataifa.  Ikumbukwe kwamba ni Mtakatifu Yohane Paulo wa II aliye anzisha siku ya vijana kunako mwaka 1984. Hadi kufikia mwisho wa maisha yake, Mtakatifu Yohane Paulo II alizidi kusisitizia vijana kila mara kuwa: wao ni matumaini ya Kanisa. Huo pia  ndiyo mwendelezo wa Baba Mtakatifu Francisko kwa vijana hao, hadi kufikia kipaumbele cha Sinodi ya Maaskofu kuhusu Vijana imani na mang’amuzi ya miito uliofanyika Oktoba 2018. Kila washiriki wa Mkutano wa siku ya vijana wameweza kugusa na kugundua njia bora ya kuishi kwa pamoja na kuadhimisha sikukuu ya Kristo aliye hai katika Kanisa na ndiyo utume wao wa kuinjilisha na kuwafanya wengine watambue nini maana ya kumfuasa Kristo ili kuweza kuwa na furaha katika maisha.

Historia, maisha, utume na changamoto alizokabiliana nazo Mtakatifu Yohane Paulo II

Historia, maisha, utume na changamoto alizokabiliana nazo Mtakatifu Yohane Paulo II katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro ni nyingi, na zaidi mateso ya kimwili, kutokana na kupigwa risasi, lakini hata msamaha alio mpatia alieye mjeruhi. Anatambua nini maana ya mateso, magonjwa uzee, ukosefu wa ajira na mambo yote yanayo mhusu binadamu. Mtakatifu Yohane Paulo II alikuwa mstari wa mbele kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya kifamilia dhidi ya sera na mikakati iliyokuwa inalenga kubomoa taasisi ya familia.  Hata hivyo umuhimu wa familia katika jamii pia ndiyo lengo na utambuzi wa Mama Kanisa, ambapo inakazia kuwa  maisha ya ndoa na familia ni kadiri ya mpango wa Mungu.

Katika hati ya Mtakatifu Yohane Paulo II anasema kwamba, Familia ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inapaswa kulindwa na kudumishwa hata kama ni kwa njia ya sadaka binafsi ya maisha. Vile vile kuhusu utetezi  wa Injili iliyo hai hasa  dhidi ya utamaduni wa kifo unaokumbatia sera za utoaji mimba, ubinafsi na hali ya kutojali wala kuguswa na utakatifu wa maisha vilikuwa ni kipaumbele pia cha Mtakatifu  Yohane Paulo II. Hatimaye katika maisha ya Mtakatifu Yohane Paulo II alikuwa na ibada kubwa kwa Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa. Katika ufupisho huo, wa maisha yake, unaweza kuona kuwa ndiyo njia kwa  viongozi wakuu wa Kanisa  kuliongoza taifa zima la watoto wa Mungu ili kufikia mapambazuko ya ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo na ambao ni kwa ajili ya wote!

MT. YOHANE PAULO II
02 April 2019, 10:45