Tarehe 21 Juni Papa atakwenda Napoli katika mkutano wa Taalimungu!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Tarehe 11 Februari 2019 Msemaji Mkuu wa mpito wa vyombo vya habari Vatican, Bwana Alessandro Gisotti ametoa taarifa kuwa Baba Mtakatifu Francisko atakwenda mjini Napoli Italia tarehe 21 Juni 2019, mahali ambapo atashiriki sehemu ya Mkutano utakao ongozwa na kauli mbiu,Taalimungu baada ya Varitatis Gaudium kwa mantiki ya kimediteranea. Ni Mkutano unaoandaliwa na Taasisi ya Kipapa ya Taalimungu Italia ya Kusini, iliyopo Napoli Italia.
Ratiba ya Baba Mtakatifu kwa siku hiyo
Ratiba ya siku hiyo inatazamiwa kuwasiri kwa Baba Mtakatifu Francisko katika mji wa Campagna mida ya saa 3.00 asubuhi masaa ya Ulaya na kati ya watakao mpokea Baba Mtakatifu ni pamoja na Kardinali Crescenzio Sepe,Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Napoli, Kansela wa Taasisi hiyo, Askofu Francesco Marino wa Jimbo Katoliki la Nola, Italia na Mkuu wa Shirika la Wajesuit, Padre Arturo Sosa Abascal. Mkutano kwa watu wote unatazamia kufanyika katika uwanja mpana mbali kidogo na Taasisi hiyo.
Kauli mbiu inayoongoza mkutano
Baba Mtakatifu Francisko ambaye ametembelea Napoli kunako tarehe 21 Machi 2015 atatoa hotuba yake inayojikita katika mada ya mkutano huo na mara baada ya hotuba hiyo itafuata chakula cha mchana na baadaye kurudi mjini Roma.
Chuo Kikuu na Kitivo ha Kanisa na muundo wa hati ya Veritatis Gaudium
Muundo wa Hati ya kitume ya Veritatis Gaudium ya Baba Mtakatifu Francisko kuhusu vyuo vikuu na Kitivo cha Kanisa,ulichapishwa na kutangazwa kunako tarehe 29 Januari 2018 ili kusaidia mchakato wa waamini kupata elimu, ujuzi na maarifa ya kisayansi kwa kuendeleza Elimu Katoliki katika sehemu mbalimbali za dunia. Baba Mtakatifu Francisko katika Hati hiyo anasema hii ni njia ya kubadilisha elimu na dunia ambayo inaweza kubadilika na Kanisa linatambua kwamba, elimu ni sehemu ya haki za msingi za binadamu kwani kila binadamu ana haki ya kupata elimu bora inayo ambatana pia na elimu ya Kikristo.