Askofu Antoine Kambanda ateuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Kigali
Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Baba Mtakatifu ameridhia maombi ya kung’atuka katika shughuli za uchungaji la Jimbo Kuu la Kigali nchini Rwanda. Ni maombi yaliyowakilishwa na Askofu Mkuu Thaddée Ntihinyurwa na wa wakati huo huo, amemteua kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo katoliki Kigali, Askofu Antoine Kambanda ambaye hadi uteuzi wake alikuwa ni askofu wa Kibungo.
Maisha ya Askofu Antoine Kambanda
Askofu Antoine Kambanda alizaliwa tarehe 10 Novemba 1958 katika jimbo Kuu katoliki la Kigali. Kwa bahati mbaya wazazi wake wote waliuwawa wakati wa vita vya mwaka 1994 na kubaki na kaka yake ambaye kwa sasa anaishi nchini Italia. Masomo yake ya hawali yalianzia nchini Burundi na Uganda na baadaye kumalizia shule ya Sekondari nchini Kenya. Alirudi katika nchi yake Rwanda mara baada ya kumaliza masomo ya Falsafa na miaka miwili ya Taalimungu katika Seminari ya Kuu ya Nyakibanda Jimbo katoliki la Butare.
Daraja la upadre-uaskofu na shughuli za utume
Alipewa daraja Takatifu la Upadre kunako tarehe 8 Septemba 1990 na Mtakatifu Yohane Pauli II wakati wa Ziara yake ya kitume nchini Rwanda mwaka huo. Na mara baada ya kupewa daraja la upadre, aliendelea na shughuli za kitume kama ifuatavyo: 1990-1993 kama Mwalimu na Gombera wa Seminari ndogo ya Ndera Kigali; 199-1999 aliendelea na Masomo yake katika Chuo cha Kipapa cha Alfonsina mjini Roma, mahalia ambapo alipata shahada ya uzamivu wa Taalimungu ya Maadili, akiwa anakaa katika Chuo cha Kipapa cha Mtakatifu Paulo; kuanzia 1999-2005 alikuwa ni Mkurugenzi wa Caritas jimbo kuu la Kigali; Mkurugenzi wa Tume ya Jimbo ya Haki na amani, Profesa wa Taalimungu Maadili katika Seminari Kuu ya Taalimungu Nyakibanda na mwalimu wa kiroho wa Seminari Kuu ya Rutongo.
2005-2006 Gombera wa Seminari Kuu ya Falasafa huko Kibgayi na 2006 Gombera wa Seminari Kuu ya Mtakatifu Caroli Borromeo huko Nyakibanda katika Jimbo la Butare. Na tarehe 7 Mei 2013 alichaguliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Askofu wa Kibungo.