Ufunguzi wa Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya vijana!
Sr. Angela Rwezaula- Vatican
Katika fursa ya kufungua Sinodi ya maaskofu, Baba Mtakatifu anatarajia kuadhimisha Misa katika Uwanja wa Mtakatifu Petro mjini Vatican 3 Oktoba 2018, na mchana katika Ukumbi wa Sinodi wataanza rasmi na sala na salam za mwanzo katika mkutano. Wakati wa shughuli za kazi ya ufunguzi, pia Katibu Mkuu wa Sinodi ataonesha kitendea kazi,yaaani Istrumentum laboris na mfumo mzima wa sinodi itakavyokuwa, pamoja na kuwakilisha sehemu ya kwanza ya mkutano.
Mababa wawili wa Sinodi kutoka China
Habari zinaeleza kuwa, katika wanaodhuria Sinodi ya vijana, ni mababa wa sinodi 267. Kwa mara ya kwanza na baada ya kutiwa saini ya mkataba wa muda kati ya Vatican na Jamhuri ya watu wa China, watakuwapo hata maaskofu wawili kutoka nchini China. Taarifa zilizotolewa kuhusu mababa hawa wawili kutoka China, ni Askofu Giuseppe Guo Jincai, wa Chengde, katika jimbo la Hebei. Alizaliwa kunako tarehe 27 Februari 1968 na kupewa daraja la uaskofu mwaka 2010, amesomea huko Prado, Lione nchini Ufaransa. Baba mwingine, ni Askofu Giovanni Battista Yang Xiaoting wa Yan'an, katika jimbo la Shaanxi. Alizaliwa kunako tarehe 9 Aprili 1964 na kupewa daraja la uaskofu kunako 2010. Shahada ya taalimungu mjini Roma 1999.
Katika Sinodi ya XV ya Maaskofu, ambayo itahitimishwa tarehe 28 Oktoba, wanaudhuria kama wasikilizaji hata vijana 34, wenye umri kuanzia 18-29 kutoka duniani kote kuwakilisha sauti ya vijana wenzao. Kwa mujibu wa Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu Mkuu wa Sinodi, wakati wa kuwakilisha kwa waandishi wa habari juu ya utaratibu mzima wa sonodi utakavyokuwa, Jumatatu Mosi Oktoba 2018 alisema, hii ni Sinodi ya tatu kuitishwa na Papa Francisko ambayo inaanzia katika misingi yake yenyewe, kwanza familia, na vijana ambao wanahakikisha wakati endelevu wa kizazi.